Akibaki Sanchez, Arsenal tunachukua ubingwa msimu huu – Madee
Msanii wa Bongo Fleva, Madee amedai kuwa msimu huu wa 2017/18 klabu yake pendwa ya Arsenal inauwezekano mkubwa kutwaa ndoo ya Ligi Kuu England (EPL) endapo mshambuliaji wa klabu hiyo, Alexis Sanchez atasalia klabuni hapo.
Madee amesema sababu za yeye kuwa na matumaini hayo ni jinsi namna ya timu yake inavyofanya usajili wa gharama ndogo huku akiamini timu yake haina presha ukilinganisha na klabu nyingine zinazotumia pesa nyingi kwenye usajili.
“Naamini kabisa ubingwa mwaka huu ni wetu, endapo Sanchez atasalia Arsenal najua tuna mashine yetu mpya Lacazette lakini bado tunamuhitaji Sanchez akamilishe amalizie safari yetu ya ubingwa mapema, tunasubiri muda tu tuchukue ndoo”,amesema Madee kwenye mahojiano yake na Bongo5.
Hata hivyo Madee ametaja timu pinzani kwa Arsenal msimu huu kuwa ni Manchester United na Manchester City huku akiiweka Chelsea kwenye nafasi ya 4 kwani amedai hajaona nguvu yao ya kutetea ubingwa msimu.
Madee kwa sasa anaetamba na ngoma yake mpya ‘Sikila’ anaamini huu ndiyo utakuwa msimu wa furaha kwa mashabiki wa Arsenal baada ya kuumia kwa kipindi kirefu.
Tazama video ya wimbo mpya wa Madee aliomshirikisha Tekno ‘Sikila’