Habari

Alichozungumza Makamu wa Rais wakati wa uzinduzi wa baraza la vijana zanzibar

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa jamii haina budi kutambua kuwa vijana wana fursa kubwa katika kuleta maendeleo ya nchi .

Makamu wa Rais aliyasema hayo wakati wa Uzinduzi wa Baraza la Vijana Zanzibar uliofanyika kwenye ukumbi wa Baraza la Wawakilishi wa Zamani Kikwajuni.

Makamu wa Rais alisema kuwa Baraza la Vijana Zanzibar ni Chombo au jukwaa litakalowavusha vijana kufikia maendeleo wanayohitaji kiuchumi, kijamii, kisiasa na kufuatana na kasi ya maendeleo ya sayansi na teknolojia Duniani.

“Ni imani yangu kuwa Baraza hili litakuza mioyo yenu ili muweze kujituma, kujiendeleza na kuwa mstari wa mbele katika kuunga mkono serikali yenu pamoja na kutetea na kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar na kuenzi fikra za Muasisi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume (Mungu amrehemu)”

Makamu wa Rais aliendelea kusema kuwa Uzinduzi wa Baraza la Vijana Zanzibar ni mwendelezo wa mawazo ya Wana Mapinduzi ya kutaka kuweka hali za wananchi kuwa sawa (Bora), na kujenga Taifa lenye Vijana Imara.

Makamu wa Rais alisisitiza kuwa ni matarajio yake kuwa Baraza la Vijana Zanzibar litaendeshwa kwa misingi ya demokrasia na sheria, kanuni na miongozo ya taasisi itakavyoelekeza.

Baraza hilo linalotokana na Sera ya Maendeleo ya Vijana ya Mwaka 2005, sera hii ndio iliyopelekea kupitishwa kwa sheria nambari 16/2016 iliyoanzisha Baraza hilo, hatua ya utekelezaji wa Mkataba wa Vijana Afrika 2006 ambapo Jamhuri ya Muungano imeridhia.

Makamu wa Rais aliwataka Vijana kuwa mstari wa mbele katika kutunza amani ya nchi, kutoa ushauri pale wakiwa na mawazo mbadala, kutengeneza mtandao na kuitumia mitandao kwa manufaa ya kuwaleta pamoja na kukemea vitendo vyote vya udhalilishwaji wa watoto na wanawake.

Aidha Makamu wa Rais aliwataka vijana hao kuwa wamoja na kujenga hali ya kujitegemea na badala kuwa tegemezi, watetezi wan chi, kuibua mawazo mapya ya maendeleo na washiriki kwa kupaza sauti katika mambo yanayowahusu.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents