Allan Kingdom: Rapper Mtanzania aliyeshirikishwa na Kanye West kwenye ngoma mpya ‘All Day’ (Details)
Kanye West anafahamika kwa kuwatoa wasanii wengi wakubwa nchini Marekani. Bila yeye leo hii hakuna mtu angekuwa anawajua Big Sean na John Legend. Na sasa kupitia ngoma yake mpya ‘All Day’, (ambayo hakuna shaka itakuwemo kwenye album yake mpya), Yeezy anamweka kwenye ramani ya muziki duniani, rapper Mtanzania aishiye Minnesota, Marekani, Allan Kingdom.
Tazama video hiyo chini kuona Kanye na Allan wakitumbuiza jana kwenye Brits Awards jijini London
https://www.youtube.com/watch?v=X8GsQhCAkcg
Hakuna mkazi wa Minnesota asiyemjua rapper huyu na infact ni supaster tayari pande hizo japo tunasikitika kuwa tumemfahamu sasa kupitia Kanye West aliyemshirikisha kwenye ngoma yake ambayo tayari inapendwa na ilivuja wiki iliyopita.
Kinachofurahisha zaidi ni kuwa Kanye amempandisha rapper huyo jana (Jumatano) kwenye Brit Awards (zenye level sawa na tuzo za Grammy za Marekani) zilizofanyika jijini London kutumbuiza ngoma hiyo.
Kanye West na Allan Kingdom wakitumbuiza kwenye Brits Awards
Tuzo hizo zimehudhuriwa na mastaa wote wakubwa unaowajua wakiwemo Kim Kardashian, Taylor Swift, Lionel Richie, Sam Smith kutaja wachache tu.
Kwa mujibu wa Star Tribune, Kanye atakuwa amemfahamu Allan kupitia mkurugenzi wake wa ubunifu, Virgil Abloh ambaye ni sehemu ya watu walio kwenye kambi ya Allan. Hakitakuwa kitu cha ajabu kama akishawishika pia kumuongeza kwenye list ya wasanii wa label yake, GOOD Music.
Allan Kingdom ni nani?
Mwaka jana mtandao wa Complex ulimjumuisha kwenye orodha ya rappers 25 wapya wa kuwaangalia mwaka 2014. Allan Kingdom ni rapper na producer wa muziki mwenye makazi yake St. Paul, Minnesota nchini Marekani.
Alizaliwa kwa jina la Allan Kyariga miaka 21 iliyopita nchini Canada na mama kutoka Tanzania pamoja na baba kutoka Afrika Kusini.
Amezunguka sana kabla ya kumaliza shule pale Woodbury High School, Minnesota.
“Naweza kuzoea kiurahisi kabisa kwenye mazingara tofauti tofauti, lakini sijawahi kuhisi kiukweli kuwa mimi ni sehemu ya jamii moja,” rapper huyo aliliambia gazeti kubwa zaidi la kila siku katika jimbo la Minnesota, Star Tribune.
Ni rapper anayekubalika mno katika jiji la St. Paul. Hadi sasa tayari ana album moja na EP nne.
Anasema mtindo wake wa muziki unachukua sana vionjo pia kutoka Afriki Mashariki kupitia muziki ambao mama yake alikuwa akisikiliza alipokuwa mdogo na kuchanganya na ladha za waimbaji wanaomuinspire kama Frank Ocean, Odd Future, Earl Sweatshirt na Kid Cudi.
Uhusiano wake na Kid Cud ni mkubwa zaidi kwakuwa mmoja wa watayarishaji wa Cud, Plain Pat, ni meneja wa Allan.
Pat aliupenda muziki wa Allan kupitia Twitter.
“Aliniambia nimetishwa sana na production yako,” anakumbushia Allan, ambaye kipindi hicho alikuwa na umri wa miaka 17.
Allan alipitia pia kusoma masuala ya sanaa kupitia Creative Arts High School ambako alikaa kwa muda kabla ya kurejea tena Woodbury. Pia amesoma masuala ya studio engineering kupitia Institute of Production & Recording huko Minneapolis.
Akiwa mtoto pekee wa wazazi wake, ametumia muda mchache mno kukaa na baba yake aliyerudi Afrika Kusini wakati Allan akiwa mtoto. Kwahiyo amelelewa zaidi na mama yake Mtanzania.
Wazazi wake walikutana wakati wakisoma kwenye chuo kikuu cha Manitoba huko Winnipeg nchini Canada na aliishi huko hadi darasa la tatu.
Mama yake Laurencia, amewahi kumleta Tanzania mara kadhaa na kumfundisha utamaduni wa nyumbani.
Allan akiwa na mama yake (kulia) na binamu zake kwenye birthday yake Jan 3 mwaka huu
Akiwataja wasanii wa Congo kama vile Koffi Olomide na Papa Wemba, Allan alisema, “Mwanzoni nilipoanza kutoa nyimbo watu walisema walikuwa wakisikia hiyo ‘influence’ na kwakweli kilikuwa ni kitu kinachotokea bila kujua (subconscious). Lakini nilifikiria, ‘OK, basi naweza kuimiliki pia. Na ndipo nikaanza kusikiliza nyimbo hizo mimi mwenyewe.”
Allan (katikati) enzi akiwa mtoto
Mama yake alikuwa na ushawishi mwingine wa pekee kwenye nyimbo za kwanza kwanza za Allan ikiwemo album yake aliyoitengeneza kupitia kanisani akiwa na umri wa miaka 11.
“Alikuwa akipitia mashairi na kusema ‘Oh, huwezi kusema hivyo.’ Alingebadilisha maneno ambayo hakuyapenda na kuweka ‘Upendo’ na ‘Yesu’ na ‘God.’
Ushawishi kutoka kwa utengenezaji wa nyimbo wa Kanye unasikika kwenye EP yake ya miaka miwili iliyopita, Trucker Music iliyodhihirisha kipaji kilichopevuka katika umri wake mdogo.
Akiongea na Papermag.com mwaka jana, Allan alisema Minnesota ni sehemu yenye wahamiaji wengi wa kigeni kutoka Afrika Mashariki na hivyo kumfanya wakati mwingine ajisikie kuwa yupo nyumbani.
“Ninaweza kusimama sehemu na kupata kitu kinachofanana na kile mama yangu angetengeneza,” alisema.
Kazi yake mpya inaitwa Future Memoirs yenye jumla ya nyimbo 12 zikiwemo ‘Wavey’ na ‘Evergreens’.
Nadhani huu sasa ni mwanzo tu wa safari ya mafanikio kimataifa wa Allan na ni jambo la kutupa moyo kwakuwa ataiweka Tanzania kwenye ramani ya kimataifa.
Shout to my family in the Serengeti grindin right now, know U can't see this but I love you.
— Allan Kingdom (@ALLANKNGDM) February 23, 2015
Tanzania inakuona Allan na inajivunia hatua uliyoifikia.