Amuua dada yake kisa wivu wa mapenzi, Jeshi la polisi latangaza kumsaka kwa udi na uvumba
Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga linamsaka kijana, Daudi Bundala kwa tuhuma za kumshambulia hadi kumuua dada yake, Suzana Bundala (21), Kwa kumpiga na kitu kizito kichwani, baada ya kumkuta akiwa amelala na mpenzi wake nyumbani kwao.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Richard Abwao, amesema limetokea Ijumaa ya wiki iliyopita katika Kijiji cha Bugoshi, Kata ya Uyogo Wilaya ya Kipolisi Ushetu.
Kamanda Abwao amesema kuwa, Chanzo cha tukio hilo ni Suzana kukutwa akiwa na mpenzi wake aitwaye, Eddy Nkimbila, nyumbani kwao kitendo kilichomchukiza mtuhumiwa na kuanza kumshambulia dada yake na kumsababishia kifo.
“Ilikuwa saa tano kamili usiku katika Kijiji cha Bugoshi ambapo Daudi Bundala alimkuta dada yake akiwa amelala na mpenzi wake Eddy Nkimbila nyumbani kwao kisha kumshambulia na kitu kizito kichwani na kumsababishia kifo,” amesema Kamanda Abwao.
Kamanda Abwao amesema mtuhumiwa alikimbia baada ya tukio hilo na juhudi za kumtafuta na kumkamata zinaendelea,
Chanzo: Nipashe