Argentina yailaza Uholanzi 4-2, fainali Argentina na Ujerumani july 13
Timu ya soka ya Argentina imejikatia tiketi ya kufuzu kwa fainali yake ya kwanza tangu mwaka 1990 baada ya kuilaza timu ya Uholanzi kwa goli 4-2, ambapo fainali itachuana na Ujerumani july 13 siku ya jumapili.
Katika mchezo huo wa nusu fainali wa jana, Argentina na Uholanzi zilitoka sare tasa baada ya muda wa kawaida na ule wa ziada kumalizika na hivyo kulazimu mechi hiyo kuamulia kwa mikwaju ya penalti.
Kipa wa Argentina Sergio Romero ndiye aliyekuwa nyota katika mechi hiyo baada ya kuokoa mikwaju miwili na kuipa Argentina Ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya Uholanzi.
Romero aliokoa mikwaju ya Ron Vlaar na Wesley Sneijder.
Wafungaji wa Argentina walikuwa ni Lionel Messi,Ezequiel Garay Sergio Aguero na kisha Maxi Rodriguez.
Kocha wa Argentina Alejandro Sabella amefurahia kufuzu kwa fainali.
Uholanzi ambayo sasa imeshindwa kutwaa kombe la dunia hata baada ya kufuzu kwa nusu fainali tatu mfululizo itachuana dhidi ya wenyeji Brazil siku ya jumamosi kuamua mshindi wa tatu.