Arsenal yamchelewesha Eden Hazard kutua Real Madrid, kilakitu kuwekwa hadharani Mei 29
Mchezaji wa klabu ya Chelsea, Eden Hazard anatarajiwa kutangazwa rasmi kuamia Real Madrid mara baada ya waajiri wake watakapocheza fainali ya michuano ya Europa League dhidi ya Arsenal Mei 29, hii ni kwa mujibu wa vyanzo vya habari kutoka nchini Ufaransa.
Kwa misimu kadhaa sasa Real imekuwa ikihusishwa kutaka kumsajili nyota huyo, na kwa sasa ipo tayari kutoa kitita cha euro milioni 100 ambayo sawa na pauni milioni 86.
Hazard amekuwa akihusishwa kuwa pendekezo la kocha wa sasa wa Real, Mfaransa Zinedine Zidane.
Kwa mujibu wa chombo cha habari L’Equipe kimeripoti kuwa, makubaliano kati ya nyota huyo mwenye umri wa miaka 28 na Real tayari yameshafanyika wiki moja iliyopita, huku taarifa ikitarajiwa kutolewa mara baada ya msimu kumalizika rasmi. Ukweli huo utawekwa wazi Mei 29, baada ya Chelsea kuikabili Arsenal huko jijini London.
Hata hivyo Chelsea imemaliza kwenye nafasi ya tatu Premier League na hivyo kufanikiwa kukata tiketi ya kufuzu kushiriki michuano ya Champions League msimu ujao.
Hazard amebakiza mwaka mmoja pekee wa kuendelea kusalia Stamford Bridge kabla ya mkataba wake kumalizika.