Asha Baraka amuuza Choki
MKURUGENZI wa African Stars Entertainment (ASET), Asha Baraka, ametaka tajiri anayetaka kumnunua mwimbaji wake nyota, Ali Choki, kujitokeza ili wakubaliane bei.
na Khadija Kalili
MKURUGENZI wa African Stars Entertainment (ASET), Asha Baraka, ametaka tajiri anayetaka kumnunua mwimbaji wake nyota, Ali Choki, kujitokeza ili wakubaliane bei.
Asha alisema mwishoni mwa wiki, kuwa kama kweli yupo mtu ambaye ameandaa donge la kuanzisha bendi huku akilenga kumnyakua Choki, ajitokeze biashara ifanyike.
Kama kweli kuna huyo wanayesema katenga sh milioni 300 ambazo ni mahsusi kwa kuanzisha bendi, huku akilenga kumnunua Choki kwa kumpa gari aina ya Baloon na fedha kiasi cha sh mil 30, ajitokeze ili amnunue hata ikibidi wanamuziki wote na hata kama jina la bendi, endapo atahitaji kufanya hivyo, alisema Asha.
Asha aliamua kutoa kauli kutokana na uvumi ulioenea jijini Dar es Salaam kuwa, kuna mtu ambaye ni mchimba madini ametenga mamilioni ya fedha kwa ajili ya kuanzisha bendi na kutangaza kumnyakua Choki na nyota wengine kadhaa.
Mimi mwenyewe nazitafuta hizo milioni 30/- ambazo nasikia ndizo zimetengwa za kumng’oa Choki, hivyo huyo mtu aje tukubaliane, nitamuuzia kila kitu, hakika kusema kweli katika hili sina mjadala, alisema Asha.
Source: Tanzania Daima