Habari

Asimia 90 ya watangazaji si wanataaluma – Dkt Mwakyembe

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harisson Mwakyembe amesema, asilimia 90 ya watangazaji wamebainika kutokuwa na sifa za kitaalamu za uandishi wa habari na utangazaji.

Hayo yamezungumzwa na Waziri Mwakyembe wakati akitoa taarifa hiyo bungeni alipokuwa anawasilisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018 ya Shilingi bilioni 28.2.

“Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imeendelea kusimamia ubora wa huduma za utangazaji kwa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye vituo vya utangazaji kwa lengo la kuhakiki vitendea kazi na ubora wa huduma zinazotolewa na vituo hivyo,” alisema Mwakyembe.

“Maeneo yaliyohakikiwa ni pamoja na studio, vyumba vya kuandaa habari, maktaba, utaratibu wa ndani wa kuandaa na kutangaza vipindi, sifa za watangazaji na waandishi wa habari na mikataba ya ajira.

“Vituo vyote vilivyokaguliwa vilionyesha ubora katika kutoa huduma kwa wasikilizaji wake katika maeneo husika, ikiwa ni pamoja na ubora wa usikivu ambao hauna miingiliano ya sauti, ubora wa vitendea kazi katika vituo, uelewa wa taratibu na sheria za utangazaji pamoja na uwezo wa kituo katika kutimiza haki na maslahi ya wafanyakazi wake.

“Lakini katika ukaguzi huo, asilimia 90 ya wafanyakazi walibainika hawana sifa stahiki katika taaluma ya uandishi wa habari na utangazaji, jambo linaloifanya iendelee kuwa changamoto kubwa katika tasnia ya habari na utangazaji nchini,” alisema Dk. Mwakyembe.

Na Emmy Mwaipopo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents