Burudani

Audio: Nimezunguka vituo vyote vya polisi sijapata chochote – Mke wa Roma

Mke wa Roma Mkatoliki, Nancy ambaye ni mama wa mtoto mmoja aitwae Ivan, amedai yeye pamoja na ndugu zake wameshazunguka kila sehemu bila mafanikio kumtafuta mume wake ambaye ametekwa usiku wa Jumatano hii akiwa studio za Tongwe Record Masaki jijini Dar es Salaam.

Akiongea na waandishi wa habari jioni hii, Nancy amesema mara ya mwisho kuzungumza na Roma ilikuwa jana saa kumi na mbili jioni.

“Mimi kama mke wa Roma mara ya mwisho niliwasiliana na mume wangu jana saa kumi na mbili jioni, akaniambia anaelekea Tongwe Records kwajili ya kazi zake za kila siku. Baada ya hapo sikuwa nampata tena kwenye simu lakini nikachukulia ni kawaida tu simu imezima, nimekuja kuamka saa 7 nikapokea simu kutoka kwa rafiki yake akaniambia uko na Roma nikamwambia hapana alikuwa Tongwe, akaniambia kuna taarifa kwenye mitandanao na mimi nikaingia nikakuta hizo taarifa kama walizopata watu wengine,” alisema Nancy.

Aliongeza, “Baada ya hapo nikaanza kutafuta watu wa kunisaidia, baadhi ya ndugu zangu wameangaika vituo vyote vya polisi Roma hayupo, hadi sasa hivi sifahamu yuko wapi, kwa ufupi sina ninachokijua wala ninachokifahamu. Jitihada zangu za kutafuta kwenye vituo vyote vya polisi nimemaliza,”

Alisema mume wake huyo hakuwai kumpatia taarifa yoyote kama anatafutwa na polisi wala ana tatizo na mtu yeyote.

Pia aliwaomba wadau mbalimbali pamoja na watanzania kwa ujumla kumuunga mkono katika jitihada za kumtafuta mume wake ambaye mpaka sasa hajulikani aliko.

Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es salaam Kamishna Simon Sirro amesema kuwa wamezipata taarifa hizo na wanazifanyia kazi.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents