Baada ya kutoa masaa 24 kwa wafanyabiashara Watanzania kuondoka Kenya, Jaguar abadili kauli “Hamkunielewa, Sikumaanisha hivyo”
Baada ya kutoa amri kwa vyombo vya dola nchini Kenya kuwafukuza wafanyabiashara wa kigeni nchini humo wakiwemo Watanzania, Hatimaye Jaguar abadili kauli kwa kusema kuwa hakumaanisha wafanyabiashara Watanzania au wale wanaotoka nchi jirani bali Wachina.
Jaguar ametoa masahihisho ya kauli yake kupitia ukurasa wake wa Twitter, kwa kusema kuwa watu wengi hawakumuelewa na hakumaanisha kuwafukuza wafanyabiashara wa nchi jirani.
“Nilikuwa na maana ya Wachina ambao ndio wamevamia soko letu na kufanya biashara za wazawa kudhorota. Mimi sipingani na wafanyabiashara wa ukata wetu kwani wanaimarisha uchumi wa pande zote,“ameandika Jaguar.
Kauli hiyo imekuja ikiwa ni siku moja imepita tangu aagize vyombo vya dola kuwavurumisha wafanyabiashara ambao sio wazawa, wanaofanya kazi kwenye jimbo lake la Starehe.