Burudani

BASATA lawachimba mkwara wasanii, redio TV na tovuti kuhusiana na nyimbo zenye matusi

Hii ni taarifa ya Baraza la Sanaa la Taifa, BASATA iliyotolewa Jumatano hii:

Forever-Young-Explicit-top

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) linawaagiza wasanii, wamiliki na waendeshaji wa wavuti, tovuti na vyombo vya habari hususan radio na runinga kuondoa na kuacha mara moja kurusha au kutangaza au kucheza nyimbo zote zenye maudhui ya kashfa, matusi, kejeli, udhalilishaji ambazo zinahatarisha kuigawa jamii ya kitanzania katika misingi yoyote hasa katika kipindi hiki Taifa linapoendelea na kampeni za kisiasa na kujiandaa na uchaguzi mkuu.

Kwa mujibu wa kifungu namba 118 (a-d) cha Sheria ya Bunge namba 9 ya Mawasiliano ya Mtandao ya mwaka 2010 ni marufuku kwa njia yoyote kwa mtu au chombo chochote kutengeneza, kuzalisha, kusambaza au kutangaza ujumbe ambao una mlengo wa matusi, dharau, uzushi au jinai kwa lengo la kutukana, kutisha, kusumbua au kushusha hadhi ya mtu mwingine.

Aidha, Sheria ya Bunge namba 4 ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015 kifungu cha 45 (1) (a-c) kinatoa mamlaka kwa taasisi au mtu yeyote anayebaini uvunjifu wa Sheria katika mitandao kutoa notisi kwa yeyote yule anayesambaza au kutangaza ujumbe au maudhui yanayovunja sheria za nchi kuacha mara moja au vinginevyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote anayekaidi.

Ni kwa msingi huu, BASATA linawaagiza wasanii, wamiliki wa wavuti, tovuti na wale wenye akaunti kwenye mitandao ya kijamii kama sound cloud, U-Tube, ITunes nk. kuondoa ndani ya siku saba (7) kuanzia siku ya kwanza ya taarifa hii nyimbo zote zinazokengeuka maadili na kubeba mlengo wa matusi, kashfa, kejeli na udhalilishaji wa watu wa kada mbalimbali wakiwemo viongozi wa kisiasa na kitaifa.

Aidha, BASATA linawakumbusha tena Wasanii wote nchini kuacha mara moja kubuni na kutengeneza kazi za Sanaa zenye kuashiria kuigawa jamii katika misingi yoyote ya kibaguzi na zaidi kutumia Sanaa kubomoa jamii badala ya kuijenga.

BASATA linawasisitiza wamiliki wa vyombo vya habari hususan radio na runinga pia watangazaji na Ma DJs kuhakikisha hawawi chanzo cha kusambaza maudhui yoyote ya Sanaa yenye mlengo wa kuibua chuki, matusi, kashfa na mgawanyiko wa Taifa.

BASATA kwa mamlaka yake chini ya Sheria namba 23 ya mwaka 1984 na yale ya Sheria ya Mawasiliano ya Posta na Mitandao ya mwaka 2010 na ile ya Makosa ya mitandao ya mwaka 2015 kwa kushirikiana na vyombo vya dola halitasita kuchukua hatua kali za kisheria na kinidhamu kwa wasanii, wamiliki wa wavuti, tovuti na vyombo vya habari ambavyo vitaendelea kutangaza na kusambaza nyimbo zenye mwelekeo wa kuhatarisha usalama, umoja na mshikamano wa Taifa.

BASATA likiwa ni msimamizi na mratibu wa sekta ya Sanaa nchini linatambua kwamba Sanaa ikitumiwa kwa ukengeufu inaweza kuwa chanzo kikuu cha machafuko, mivurugano na kupotea kwa amani nchini. Hivyo umakini unahitajika miongoni mwa wasanii katika kuzingatia weledi, maadili, uzalendo kwa taifa na kuitumia Sanaa kama chombo cha kujenga jamii yenye kuzingatia maadili.

SANAA NI KAZI TUIKUZE, TUILINDE NA KUITHAMINI

Godfrey L. Mngereza
KATIBU MTENDAJI, BASATA

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents