Blanc aingia kwenye orodha ya makocha wanaowaniwa kuifundisha United msimu ujao
Manchester United ni miongoni mwa timu za Uingereza zilizotumia fedha nyingi kufanya usajili msimu wa 2015-2016, lakini bado maji yanazidi unga kwa kocha, Louis Van Gaal.
Kocha wa timu ya PSG, Laurent Blanc ambaye pia aliwahi kuichezea timu ya Manchester United kwa misimu miwili ameingia kwenye orodha ya makocha ambao wanawaniwa na uongozi wa timu hiyo kuweza kuchukua mikoba ya Van Gaal, limesema gazeti la Daily Star.
Blanc ambaye ameisaidia PSG kuchukua kombe la ligi kuu ya Ufaransa (Ligue 1) mara mbili mfululizo, pia msimu huu amefanikiwa kuingia kwenye robo fainali ya ligi ya mabingwa Ulaya baada ya kuitupa nje timu ya Chelsea kwenye mashindano hayo.
Makocha wengine ambao wamewahi kutajwa kuchukua mikoba ya Van Gaal msimu ujao ni pamoja na aliyewahi kuwa kocha wa Chelsea, Jose Mourinho na Ryan Giggs.