Bonta: Naachana na hip hop, ninaingia rasmi kwenye Bongo Flava
Rapper wa kundi la Weusi, Bonta Maarifa ameamua kuchukua kile kinachoonekana kuwa ni maamuzi magumu.
Bonta amedai kuwa ameamua kuachana na hip hop na sasa ataanza kufanya Bongo Flava. “Nipo kwenye huu muziki wa HPHP toka mwaka 1997 mpaka leo ni takribani miaka 15,” yanasema maelezo ya Bonta ambayo Bongo5 imeyapata.
“Nimefanya ngoma mingi sana eg MATUSI, MTI WENYE MATUNDA, NAUZA KURA, MAUWONGO, B3, MAARIFA, NYERERE, MAKTABA, WALAUMIWA, MTAANI WATU BUU, MACHO YANGU nk. Sasa nimeamuwa kubadilika rasmi na kuingia kwenye muziki wa BONGO FLEVA nikifata kwa karibu kabisa nyayo za Jaffarai, Ney wa Mitego, Cyrill, Shetta etc,” ameongeza.
“Wengi wataona kama nimesaliti HIPHOP la hasha naomba wanisamehe!! na najua marapa wengi watafurahia kuskia nimeanza kuimba BONGO FLEVA wakiamini upinzani unapungua, waambie wasianze kujipongeza muda bado!! ningependa niimbe RnB kama Ben pol, Damian, Jux au Rama D sema ile ni ngumu sana na inahitaji ufundi, basi mi ntaimba hii hii ya kubahatisha melody matata maneno 2 tatu watu kati. Kwa kuanza nitaachia wimbo wangu mpya unaoitwa MAPENZI MATAMU!! Naomba nisihukumiwe mpaka hii ngoma itoke.”
Bonta amesema Mapenzi Matamu itatoka hivi karibuni.