Brazil kuleta teknolojia ya mafuta kutoka kwa miwa
Serikali ya Brazil imesema ina nia ya kuleta nchini teknolojia ya kutengeneza mafuta ya mabaki ya miwa yanayoweza kutumika kama mbadala wa petroli. Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana
Maulid Ahmed
Serikali ya Brazil imesema ina nia ya kuleta nchini teknolojia ya kutengeneza mafuta ya mabaki ya miwa yanayoweza kutumika kama mbadala wa petroli. Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana.
Balozi wa Brazil nchini, Appio Claudio Acquarone alisema kuwa serikali yake imeshaanzisha wakala wa kampuni ya utafiti wa kilimo (EMBRAPA) ambapo itakuwa inafungua ofisi zake katika nchi za Afrika kwa lengo la kusaidia kuhamisha teknolojia hiyo.
Balozi huyo alisema tayari wameshafungua ofisi mjini Accra, Ghana ambako aliongeza, wiki iliyopita mwakilishi wa kampuni hiyo alikuja nchini, sisi tunaona kuna uwezekano wa teknolojia hii kuletwa hapa kwani hata Tanzania yenyewe imeonyesha nia ya kutaka teknolojia hii.
Nchini Brazil, asilimia 45 ya magari yote yanatumia mafuta hayo ya mabaki ya miwa. Asilimia 52 ya tani milioni 300 ya miwa inayozalishwa nchini humo inakwenda kutengeneza mafuta hayo na inayobaki inatengenezewa sukari. Lita 7,000 za mafuta ya miwa hutengenezwa kutokana na hekta moja ya miwa.
Balozi huyo alisema hekta milioni tatu za ardhi yenye rutuba nchini humo inatumika kwa ajili ya kilimo cha uzalishaji wa mafuta hayo ya miwa na kuongeza, hatuna sababu ya kutumia ardhi ya misitu ya Amazon kwa ajili ya kilimo cha mafuta hayo ya miwa.
Umbali wa eneo kunapozalishwa mafuta ya miwa na msitu wa Amazon ni kilometa 2,500 na hata kama tukitaka kuzalisha mafuta hayo zaidi tutahitaji hekta milioni sita ambazo zinapatikana katika eneo hilohilo. Brazil ilianza kuzalisha mafuta ya mabaki ya miwa kwenye miaka ya 1970 baada ya kuona inatumia fedha nyingi kuagiza petroli kutoka nchi za Mashariki ya Kati.
Source: Habari Leo