Habari

Bunge la Uingereza laukataa mpango wa May kujiondoa kwenye umoja wa Ulaya kwa mara ya pili zikiwa zimesalia siku 17, Wananchi waandamana barabarani wakifurahia (+ Video)

Mpango wa Theresa May wa Uingereza kujiondoa katika Umoja wa Ulaya umepingwa na wabunge kwa mara ya pili huku zikiwa zimesalia siku 17 hadi muda wa taifa hilo kujitoa katika EU.

Kwa mujibu wa BBC. Wabunge walipiga kura kupinga mpango wa waziri mkuu huyo kwa kura 149 – kiwango kidogo ikilinganishwa na kura zilizopigwa Januari.

Bi May amesema wabunge sasa watapiga kura iwapo Uingereza iondoke katika EU bila ya mpango na iwapo hatua hiyo itashindwa, kura ya iwapo mpango mzima wa kujiondoa – Brexit uahirishwe.

Waziri mkuu aliwasilisha ombi la dakika ya mwisho kwa wabunge waunge mkono mpango wake baada ya kupata hakikisho kisheria kuhusu msimamo wa Ireland kuhusu kujitoa katika EU.

Lakini licha ya kuwashawishi wabunge 40 wa chama cha Conservative, haikutosha kikamilifu kubadili pigo la kura ya ushindi wa kihistoria dhidi ya mpango wake mnamo Januari.

Katika taarifa yake baada ya kupata pigo hilo, May amesema: “Naendelea kuamini kwamba kwa kiasi kikubwa matokeo mazuri ni Uingereza kuondoka katika Umoja wa Ulaya katika namna nzuri na kwa mpango.

“Na kwamba makubaliano tuliyoyajadili ni bora na ya pekee tulio nayo.”

Mpango wa Bi May ni upi?

Akifafanua mpango wake, amesema wabunge watarudi tena kupiga kura Jumatano kuhusu iwapo Uingereza inastahili kuondoka EU na mpango au bila mpango.

Iwapo watapiga kura kupinga mpango , watapiga tena kura siku inayofuata kuhusu iwapo kuidhinisha kurefushwa kwa kipengee cha Article 50 – mfumo wa sheria utakao iondoa Uingereza katika EU kufikia Machi 29.

Bi May amesema wabunge itabidi waamue iwapo wanataka kuahirisha Brexit, kuandaa kura nyingine ya maoni au iwapo “wanataka kuondoka na mpango lakini sio mpango ulioko”.

Nini kinachofuata?

  • Wabunge watapiga kura tena kuhusu iwapo Uingereza ijitoe katika Umoja wa Ulaya bila ya mpango.
  • Kura inatarajiwa leo Jumatano Machi 13.
  • Iwapo wabunge wataunga mkono kujitoa bila ya mpango, watapiga kura tena Alhamisi kuhusu kuahirisha Brexit.
  • Iwapo wataunga mkono kuahirishwa kwa Brexit, May ataomba kurefushwa kwa kifungu cha sheria maarufu Article 50 kutoka kwa EU.
  • Iwapo mataifa mengine yatakubali ombi hilo, Brexit itaahirishwa.

Theresa May anasema hii haitopita miezi mitatu.

May amesema kuondoka bila ya mpango kunasalia msimamo uliopo kwa Uingereza lakini Downing Street imesema atawaarifu wabunge iwapo atapiga kura kupinga kutokuwepo mpango atakapofungua mjadala bungeni Jumatano.

Waziri mkuu hakueleza iwapo anafikiria kujiuzulu baada ya pigo hili kwasbaabu serikali anayoiongoza hivi karibuni ilishinda kura ya kutokuwa na imani naye bungeni, ameeleza msemaji wa May.

Hana mpango wa kurudi Brussels kupata ushauri zaidi, kama alivyowaambia wabunge, bado anafikiria mpango wake ndio bora na wa kipekee uliopo, ameongeza msemaji huyo.

By Ally Juma.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents