Michezo

CEO wa Simba, Senzo Kufanya mageuzi ya uongozi, ayataja maeneo matano ”Nimeazimia kusimamia uwazi”

Mkurugenzi Mtendaji wa Simba SC, Senzo Mazingiza amesema ameazimia kufanya mageuzi ya uongozi ambayo yanalenga kuisuka klabu hiyo katika mzamo mpya wa kitaalamu.

“Kwa upande wangu imekuwa safari fupi kufika hatua hii. Hata hivyo najivunia kusema wazi kwamba ajenda ya mabadiliko bado inaendelea na tunafanya kila liwezekanalo kuhakikisha kuwa klabu ya soka ya Simba inapiga hatua kubwa zaidi kisoka.”-  Senzo.

Senzo Mazingiza ameongeza kuwa “Nina uhakika kwamba waanzilishi wa klabu hii wanafurahia kuona klabu inafanya mageuzi muhimu ambayo yataisaidia kuifikisha hatua ya juu zaidi na kuhakikisha kuwa Simba inakuwa moja ya timu bora katika soka la barani Afrika. Siku chache ambazo nimekuwepo nchini zimenifungua macho na nafurahi kwamba nimekuta gari moshi likiwa tayari safarini na mimi nimekuwa mwongozaji. Soka ni kitu cha pekee katika kila nchi na kila bara, nina hakika pia ndivyo ilivyo hapa Tanzania.”

“Tegemeeni mageuzi kadhaa ndani ya uongozi. Mageuzi haya yamelenga katika kuisuka klabu katika mtazamo mpya wa kitaalamu. Nimeazimia kusimamia uwazi na uongozi jumuishi na wa kitaalamu katika mtindo wangu wa uongozi.”

“Yafuatayo ni maeneo muhimu ambayo nimedhamiria kuyaimarisha nikiwa kama CEO. (1) Marekebisho ya muundo wa ndani wa Uongozi, tunahitaji kuwa na muundo huru na wa kitaalamu wa uongozi wa kuiendesha klabu hii.”

“(2) Mabadiliko ya kisoka, hii itahusu usajili wa wachezaji na benchi la ufundi. (3) Ukuzaji wa Simba kama brandi ya mauzo ndani ya EA na sehemu zingine za Afrika. Tunahitaji kuitangaza Simba duniani kwa kufanya matangazo kwa juhudi kubwa.”- CEO Senzo.

“(3) Usimamizi wa mali za klabu zilizopo. (4) Maendeleo ya vitengo mbalimbali vya biashara. Upanuzi wa vyanzo vyote vya mapato na kubuni njia zingine za kuingiza mapato nje ya kutegemea wahisani na makusanyo ya uwanjani.”

“(5) Kuwafanya mashabiki kuwa wateja. Simba ni klabu yenye mashabiki wengi. Tunahitaji kubuni miradi itakayoifaidisha klabu, mashabiki na wanachama wetu kwa kuhakikisha kuwa uhusiano baina yao na klabu unakuwa zaidi na kufikia kuwa wateja wa klabu”- CEO Senzo.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents