Chipolopolo yadai kutwaa ushindi
Kocha wa Timu ya Zambia Herve Renard anaheshimu timu ya Kilimanjaro Stars na anajipanga kikamilifu kuhakikisha anaibuka na ushindi katika mchezo wa ufunguzi wa mashindano ya kombe la chalenji, CECAFA.
Akizungumza katika uwanja wa Karume baada ya mazoezi ya timu yake maarufu kama Chipolopolo, Renard alisema”Tumejiandaa kikamilifu kushinda ingawa mashindano haya yatakuwa magumu msimu huu’.
‘Tunaheshimu Tanzania licha ya kushuka katika viwango vya soka vya FIFA kwani kila timu imejiandaa kikamilifu. Hakuna sababu ya kudharau timu yoyote.’
Kocha huyo hakuwa tayari kusema ni kundi gani gumu kati yao waliyopangwa kwa mashindano hayo wala hakuwa tayari kusema timu ipi inamtisha.
Hata hivyo kama ilivyo kwa kila kocha makini, Renard anajipa moyo na kusema Chipolopolo ambao niwaalikwa kwenye mashindano haya watarejea Zambia na ubingwa kwani hawakuja kutalii Tanzania.
Bongo5 jana ilishuhudia timu hiyo ikifanya mazoezi katika uwanja wa Karume majira ya saa nane mchana.