Burudani

Dk Shika apewe nafasi Tanzania ya Viwanda ya Rais Magufuli – Kala Jeremiah

Msanii wa muziki wa Hip Hop, Kala Jeremiah amewataka watanzania wasimchukulie poa,  Dk Louis Shika ambaye hivi karibuni aliingia kwenye headline baada ya kushindwa kutoa asilimia 25 ya mnada wa nyumba za Lugumi muda mchache baada ya kushinda mnada huo.

DK. Louis ambaye anatamba mtaani kwa kauli yake aliyoitumia siku hiyo ya mnada ‘900 naona inafaa’ alikamatwa na Jeshi la Polisi muda mchache baada ya kushindwa kulipa pesa hizo lakini baada ya siku tatu aliachiwa kwa dhamana.

Baada ya kuachiwa, alifanya mahojiano na baadhi ya vyombo vya habari ambapo alifungaka mambo mengi ambayo yaliwafanya watu wengi waone ana kitu ndani yake.

Rapa Kala Jeremiah alikuwa ni mmoja  kati watu ambayo walishangazwa na uwezo wa Dk. Louis baada ya kumsikia katika mahojiano mbalimbali na kusema kuwa mzee huyo anafaa kuisaidia serikali katika mambo ya viwanda.

Akiongea na Bongo5 Ijumaa hii, Kala amedai Dk. Louis anaonekana ni msomi wa masuala ya kemikali na viwanda hivyo akipewa nafasi katika serikali ya Rais Magufuli anaweza kufanya kitu kikubwa na kuisaidia nchi yake..

“Kuna mambo mengi nimegundua kutoka kwa yule mzee, kwanza jinsi alivyoteseka nchini Urusi, amekosa faraja kwa muda mrefu kutokana na mambo yaliyomkuta, anahitaji upendo wa Watanzania baada ya kuukosa upendo kwa miaka mingi, aliyoyapitia kibinadamu lazima aathirike kisaikolojia kwa sababu ishu ya kupondwa vidole mpaka vikapondeka ni jambo zito sana. Kwa mimi binafsi nawaomba watanzania wamuombee pamoja na kumpatia maneno ya faraja ili na yeye apate furaha ambayo aliikosa kwa miaka mingi,” alisema Kala.

“Kwenye suala la elimu sina shaka naye yule ni msomi mbobezi kabisa kama unavyosikia ni Dk. Shika, yule ni daktari na hakuna mtanzania ambaye anabisha kwenye hilo, wakati anazungumza, anazungumza sana masuala ya viwanda na Rais wetu Magufuli anahitaji watu kama hawa ambao tayari wanautaalamu kwa muda mrefu wa masuala ya viwanda kwahiyo kama akitumika kama mshauri katika Tanzania ya Viwanda huweza kukapata kitu fulani ambacho kitasaidia Tanzania yetu,”

Rapa huyo amesema ishu ya Dk. Shika na nyumba za Lugumi ni suala ambalo halijakaa wazi kama ni kweli alikuwa anataka kununua nyumba hizo au la!.

“Mimi naweza kusema DK Shika huwenda ana matatizo ya kisaikolojia ndio maana nasema hayo yote huwenda yametokea kutokana na tatizo lake na sio ishu za kiki kama baadhi ya watu wanavyodai, huyo akipatiwa mwanasaikolojia akawa sawa anaweza kufanya kitu fulani kwaajili ya Tanzania yetu,” aliongeza Kala.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents