Dkt. Mengi kujenga kiwanda cha simu janja ‘Smartphone’ cha kwanza Tanzania, zitakuwa na sifa hii ya kipekee duniani
Kampuni ya IPP imetangaza kuanza ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza simu za smartphone, zitakazokuwa na uwezo wa kukaa na chaji kwa muda wa wiki moja, kitu ambacho hakuna Smartphone duniani yenye uwezo wa kukaa na chaji kwa muda mrefu kama huo.
Akiongea na Waandishi wa Habari leo Jijini Dar Es Salaam, Mwenyekiti Mtendaji wa makampuni ya IPP Dkt. Reginald Mengi amesema smartphone hizo zitakuwa za bei rahisi na kukaa na chaji wiki nzima.
“Simu zitakazotengenezwa na IPP TouchMate zitakuwa na uwezo wa kukaa na chaji kwa muda wa wiki moja na lengo litakuwa ni kuendana na mazingira ya maisha halisi ya Tanzania”, amesema Dkt. Mengi.
Dkt. Mengi amesema kiwanda hicho kitakuwa na mchango mkubwa kwenye uchumi na sehemu kubwa ya watakaoajiriwa ni watu wenye ulemavu.
Tayari ufungaji mitambo kwenye kiwanda hicho kitakachojulikana kama IPP TouchMate umeshaanza ambapo mbali ya simu, bidhaa nyingine zitakazotengenezwa ni pamoja na Tablet, Kompyuta mpakato, headphones pamoja na bidhaa za kielektroniki za majumbani pamoja na vipuri vyake.