Michezo

Eymael akerwa na Morrison kutembea juu ya mpira ”Kitendo alichofanya ni kuwakosea heshima wapinzani”

Kocha wa klabu ya Yanga Mbelgiji, Luc Eymael amesema kuwa hajavutiwa na kitendo alichofanya winga wake, Bernard Morrison cha kutembea juu ya mpira kwenye mchezo wa Kombe la FA dhidi ya Tanzania Prisons.

Luc Eymael amesema Mghana huyo, Morrison kitendo alichofanya ni kuwakosea heshima wapinzani wao, na kamwe havutiwi na hivyo vitu.

”Nilimwambia kuwa sipendi, nafahamu mashabiki wanapenda lakini nilimwambia sipendi, nilimwambia asifanye hivyo tena, kama anataka kufanya hivyo basi afanye dakika za mwisho kwa sababu sihitaji watu waanze kuwacheka wengine.” Amesema Luc

Luc Eymael ameongeza kuwa ”Kweli sipendi, ukifanya hivyo Ulaya unaweza kupata majeraha, hivi umeshawahi kumuona Mo Salah akifanya hivyo, Sadio Mane anafanya hivyo ?.”

”Kwa hiyo nilimwambia Morrison, kama watu wanampenda Mane, Salah, Messi. Nafahamu kwa Afrika wanapenda hivyo lakini mimi sipendi kuona watu wakichekana. Nilimwambia watu unawafurahisha lakini kwangu mimi ni kuwakosea heshima wapinzani wetu.”

Eymael alisema huwezi kukuta washambuliaji wakubwa dunia wakifanya vitendo kama hivyo huku akiwatolea mfano Sadio Mane, Salah na Lionel Messi.

Bernard Morrison alionesha kiwango kikubwa kwenye mechi hiyo ya kombe la FA na kufanikiwa kufunga bao lake la kwanza tangu ajiunge na wanajangwani hao huku ukiwa ni mchezo wake wa pili ambapo Yanga iliibuka na ushindi wa jumla ya mabao 2 – 0 uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents