Siasa

Fahamu jinsi wa ushindi wa Joe Biden unavyowatia tumbo joto viongozi wa Uarabuni (+Video)

Itabidi unisamehe ikiwa ninaonekana kuvurugika kidogo,” alisema balozi wa Saudi Arabia nchini Uingereza huku macho yake yakiangaza kwa simu ya mkononi. “Nafuatilia matokeo ya uchaguzi katika jimbo la Wisconsin.”

Hiyo ilikuwa siku nane zilizopita, kabla haijabainika ni nani atakayeingia Ikulu White House mwezi Januari mwakani.

Wakati Joe Biden alipotangazwa mshindi, uongozi wa Saudia mjini Riyadh ulichukuwa muda kujibu ikilinganishwa na jinsi ulivyofanya wakati Donald Trump alipochaguliwa.

Hii haishangazi: walikuwa wamepoteza rafiki muhimu.

Ushindi wa Bwana Biden sasa unaweza kuwa na athari kwa Saudi Arabia na mataifa mengine ya Ghuba.

Ushirikiano wa kimkakati wa Marekani katika eneo hilo ulianza mnamo mwaka 1945 na unatarajiwa kudumu, lakini mabadadiliko ya utawala unaokuja huenda yasipokelewe na wote katika miji mikuu ya Ghuba

Kumpoteza mshirika mkuu

Rais Trump alikuwa mshirika mkuu na msaidizi wa familia tawala ya Saudi Arabia

Alichagua Riyadh kuwa kituo cha kwanza cha ziara yake Kama rais baada ya kuchukuwa hatamu ya uongozi mwaka 2017.

Mume wa binti yake, Jared Kushner alibuni ushirikiano wa karibu wa kikazi na mwanamfalme Mohammed bin Salman.

Wakati ambao mashirika makuu ya ujasusi katika nchi za Ulaya yalishuku mwanamfalme huyo huenda alihusika na mauaji ya mwanahabari Jamal Khashoggi 2018, Rais Trump alijiepusha na hatua ya kumlaumu moja kwa moja

Saudia ndio iliokuwa kituo cha kwanza cha rais Donald Trump alipochukua madaraka
Saudia ndio iliokuwa kituo cha kwanza cha rais Donald Trump alipochukua madaraka

Bwana Trump pia alikataa wito wa Congress wa kusitisha kuiuzia silaha Saudia.

Kwa kuzingatia hilo Saudi Arabia, Muungano wa Falme za Kiarabu na Bahrain, unakaribia kumpoteza mshirika mkuu katika Ikulu ya White House.

Mambo mengi huenda yasibadilike lakini haya hapa baadhi ya mambo ambayo huenda yakabadilika.

Vita vya Yemen

Rais Barack Obama, ambaye Bwana Biden alihudumu chini yake kama makamu wa rais kwa miaka minane, hakupendelea mwenendo wa Saudi Arabia nchini Yemen hasa dhidi ya waasi wa Kihouthi.

Kufikia wakati anaondoka madarakani, makabiliano ya angani yamekuwa yakiendelea kwa karibu miaka miwili huku majeshi yakipata ufanisi mdogo, kusababisha uharibifu mkubwa wa miundo mbinu ya nchini na kuwaatthiri vibaya raia.

Muungano wa wanajeshi wanaoungwa mkono na saudia unaunga mkono vikosi vinavyoungwa mkono kstika serikali ya Yemen
Muungano wa wanajeshi wanaoungwa mkono na saudia unaunga mkono vikosi vinavyoungwa mkono kstika serikali ya Yemen

Kutokana na sababu hizo za msingi, Rais Obama alipunguza majeshi ya Marekani nchini humo na msaada wa kiintelijensia kwa Saudia.

Utawala wa Trump ilibadili hatua hiyo nakupatia Saudi Arabia uwezo mkubwa katika vita vya Yemen.

Sasa inaonekana hatua hiyo itaangaziwa tena, huku Bwana Biden akinukuliwa kusema kwamba “atakomesha msaada wa Marekani katika vita vyaYemen vinavyoongozwa na Saudia na kuagiza tathmini mpya ya uhusiano wetu na Saudi Arabia”.

Shinikizo kutoka kwa utawala wa Biden unaoingia madarakani dhidi ya Saudia na washirika wake wa Yemeni kuwataka wamalize mzozo sasa huenda zikaongezeka

Saudia na washirika wake, walibaini hivi karibuni kwamba mzozo wa Yemen hauwezi kumalizwa kupitia makabiliano ya kijeshi na wamekuwa wakitafuta njia ya kujiondoa kistaarabu hali ambayo haitwaacha waasi wa Kihouthi mahali walipokuwa wakati vita vya angani vilipoanza mwezi Machi mwaka 2015.

Iran

Ushindi mkubwa wa utawala wa Rais Obama Katika eneo la Mashariki ya Kati ni kufikiwa kwa mkataba wa kimataifa wa nyuklia – unaofahamika kama mpango wa pamoja wa utekelezaji (JCPOA).

Mpango huo ulichangia Iran kuondolewa vikwazo kwa masharti ya nchi hiyo kudhibiti shughuli zake za nyuklia na kuchunguzwa kwa kiwanda chake cha nyuklia.

Rais Trump alitaja mkataba huo kuwa “mbaya zaidi kuafikiwa” na kuondoa Marekani katika makubaliano hayo.

Sasa, mrithi wake anaoneka anajiandaa kuirudisha Marekani katika makubaliano hayo kwa njia fulani.

Saudia iliishutumu Iran kwa kutekeleza shambulio la ndege isio na rubani katika hifadhi zake mbili za mafuta 2019- madai ambayo Iran Inakana
Saudia iliishutumu Iran kwa kutekeleza shambulio la ndege isio na rubani katika hifadhi zake mbili za mafuta 2019- madai ambayo Iran Inakana

Qatar

Qatar ni mwenyeji wa kambi maalum ya jeshi la angani la Marekani – Al-Udeid ambayo ni muhimu sana katika eneo la mashariki ya kati.

Kuanzia hapo, Marekani inaelekeza oparesheni zake zote katika eneo hilo, kutoka Syria hadi Afghanistan.

Lakini bado Qatar inakabiliwa na vikwazo kutoka kwa nchi za Uarabuni – Saudi Arabia, UAE, Bahrain na Misri – ambazo zimekasirishwa na hatua yake ya kuunga mkono kisiasa mavuguvugu kama Muslim Brotherhood

Rais Donald Trump alimualika Emir wa Qatar Sheikh Tamim Al Thani katika Ikulu ya Whitehouse mwaka uliopita
Rais Donald Trump alimualika Emir wa Qatar Sheikh Tamim Al Thani katika Ikulu ya Whitehouse mwaka uliopita

Ususiaji huo ulianza muda mfupi baada ya utawala wa Rais Trump mjini Riyadh mwaka 2017, nchi hizo tatu zilidhani anaziunga mkono.

Awali, Bw Trump aliunga mkono hatua hiyo hadharani hadi alipofafanuliwa kuwa Qatar pia ni mshirika wa Marekani na kwamba Al-Udaid ilikuwa muhimu kwa kitengo cha ulinzi cha Marekani.

Utawala wa Rais mteule Joe Biden huenda ukashinikiza mzozo huo uliopo baina ya mataifa hayo ya ghuba kutulizwa .Hatua hiyo haijachukuliwa kwa maslahi ya Marekani, na bilashaka sio kwa maslahi ya nchi za Ghuba.

Haki za binadamu

Nchi kadhaa za Ghuba zina rekodi mbaya ya ukiukaji wa haki za binadamu, lakini Rais Trump hakuonesha wala kuwakashifu washirika wake wa Uarabuni.

Huduma ya Kijasusi ya Marekani ilihitimisha kwamba mwanamfalme wa Saudia aliagiza mauaji ya Jamal Khashoggi
Huduma ya Kijasusi ya Marekani ilihitimisha kwamba mwanamfalme wa Saudia aliagiza mauaji ya Jamal Khashoggi

Alihoji kuwa mipango, biashara na maslahi ya Marekani ilikuwa na umuhimu mkubwa kuliko wanaharakati wa wanawake waliofungwa jela; madai ya unyanyasaji wa wafanyakazi wa kigeni nchini Qatar; Ama ukweli kwamba mwezi Oktoba mwaka 2018 maafisa wa usalama kutoka serikali ya Saudi walitumia ndege rasmi kusafiri hadi Istanbul kutekeleza mauaji yaliyokuwa yamepangwa ya mkosoaji mkubwa wa Saudi Arabia Jamal Khashoggi, ambaye mwili wake haujawahi kupatikana hadi wa leo.

Rais mteule Joe Biden na utawala wake huenda wakawawajibisha.

https://www.instagram.com/tv/CHfaCpWBCM0/

https://www.instagram.com/tv/CHfaCpWBCM0/

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents