HabariUncategorized

Hakuna bomoabomoa ya karne Dar – RC Makonda

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda amewaondoa hofu wananchi wa mkoani humo kwamba hakuna bomoabomoa yoyote ya karne itakayofanyika ndani ya mkoa huo bila kuzingatia tarabitu za kufanya hivyo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotelewa na ofisi ya mkuu huyo,  imeeleza kuwa serikali imeendelea na ratiba za kurasimisha makazi.

” Mimi Paul Makonda nikiwa Mkuu wenu wa Mkoa na mtumishi wa serikali ya awamu ya tano, napenda kuwataarifu kwamba serikali hii inayoongozwa na Mhe Rais, Dkt. John Pombe Magufuli haivunji nyumba ya mtu bali inaendelea kurasimisha makazi kama ambavyo ilifanya kimara kwa kuwapatia Hati elfu Sita (6000) kwa Wananchi waliokuwa wamejenga kwenye makazi yasiyo rasmi, jitihada zinaendelea na ndivyo itakayofanyika tarehe 27/10/2017 kwa Wananchi waliojenga katika maeneo ya makongo juu,” alisema Mkuu huyo kupitia taarifa hiyo.

“Naomba niseme, na kama nimemuelewa vizuri alichokisema Mhe William Lukuvi ambae ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na maendeleo ya Makazi ni kuwa wananchi wasiendelee kujenga bila vibali vya ujenzi jambo ambalo linawanyima haki yao ya kukopeshwa, kulipa kodi ya majengo, na mwishoni kuwa na miji isiyopangwa vizuri,”aliongeza RC.

“Naomba kukiri kuwa apo awali kulikuwa na changamoto ya upatikanaji wa vibali vya ujenzi jambo ambalo haliwezi kuwa Adhabu kwa Wananchi waliojenga miaka ya nyuma iliyopita kwani ilifika hatua Mwananchi ana Hati ya Kiwanja chake na amekamikisha michoro kwa Mujibu wa Sheria na ana fedha za kuanza Ujenzi kwa ajili ya Makazi ya kuishi, unakuta Mwananchi huyo analazimika kufuatilia manispaa kwa zaidi ya miaka miwili mpaka mitatu bila kupata kibali cha ujenzi na hata akipata kibali baada ya miaka Mitatu na kuanza ujenzi, unakuta ndani ya muda mfupi watakuja baadhi ya watu wa osha kumsimamisha kwa madai hawana taarifa ya ujenzi jambo linalotengeneza mianya ya Rushwa, akimalizana na watu wa osha Wanakuja baadhi ya watu wa kikosi cha zimamoto (fire) nao inabidi atafute utaratibu wa kumalizana nao, jambo linalokera wananchi na kuwafanya wakose hamasa ya Kutafuta vibali vya ujenzi na Hatimae kujenga kiholela,” alifafanua zaidi.

TULICHOFANYA KAMA MKOA

Kutokana na sababu hizo na changamoto nilizozielezea hapo juu, serikali ya Mkoa tulifanya kikao na wataalamu wa Ardhi na nikatoa maelekezo kuwa vitengo vyote nane vinanavyohusika na Utoaji wa vibali vya ujenzi *VINAPASWA* kuwa na mfumo Mmoja wa mawasiliano (one stop center) ili Mwananchi atakapoomba kibali cha ujenzi Idara zote nane zifikiwe kwa wakati Mmoja na kupunguza usumbufu wa Mwananchi kwenda kufuatilia vibali na wakati mwingine unaambiwa wahusika hawapo.

Ili mfumo huo uanze kufanya kazi wataalamu wangu walihitaji vitendea kazi ambavyo nimewawezesha vifaa hivyo zikiwemo *Computer Hamsini (50)* katika manispaa zote za Mkoa wa Dar es Salaam na kuwataka kutoa vibali ndani ya mwezi Mmoja tangu kupokea maombi kutoka kwa Mwananchi tofauti na awali ambapo Mwananchi alikuwa akichukua muda wa miaka miwili kufuatilia kibali cha ujenzi, lengo Likiwa kuwawezesha wananchi kufuata Sheria ili kuendana na Mpango wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na makazi Chini ya _Mhe William Lukuvi_ katika kuhakikisha tunapanga miji yetu.

Kwa maelezo Haya mafupi, Naomba niseme kwenye Mkoa wa Dar es Salaam *HAPATAKUWA* na bomoa bomoa ya *KARNE* wala Nyumba ya mtu kuvunjwa *ISIPOKUWA* wananchi wanaojenga sasa ni vyema wakafuata utaratibu kama alivyoelekeza Mhe William Lukuvi waziri wa Ardhi, Nyumba na maendeleo ya Makazi, ili kuepuka kuvunjiwa Nyumba ambayo umeijenga kwa jasho jingi, na kujinyima uku ukikesha ili utimize ndoto ya kuwa na makazi bora.

Niwatakie kazi njema, na kwa pamoja tushirikiane katika Kupanga na kuendeleza Mkoa wetu wa Dar es Salaam kwa ajili ya Maendeleo ya Taifa na vizazi vyetu.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents