Hanscana adai studio ya video anayojenga itakuwa kubwa zaidi Afrika Mashariki
Muongozaji wa video na mshindi wa Tuzo za Watu, Hanscana amesema studio ya video anayoijenga itakuwa kubwa zaidi Afrika Mashariki.
Hanscana ameiambia Bongo5 kuwa ujenzi wa studio hiyo umeanza tayari na unatarajia kukamilika muda wowote.
“Studio ninayojenga ni studio kubwa ambayo haijawahi kutokea Afrika Mashariki,” amesema. “Hata ukitaka nije nikuonyeshe studio yangu inavyojenga mwenyewe utakubali. Ina thamani ya pesa nyingi sana na inaongezeka kadri inavyoendelea kujengwa.”
Hansana amesema studio hiyo inatarajia kuleta mapinduzi makubwa ya muziki kutokana na mataifa mengi kuiangalia Tanzania kwenye masuala ya muziki.
“Tanzania ndio tunaangaliwa sasa hivi kimuziki, tunaogopwa, ndio maana unaona sasa hivi wasanii wengi wa kimataifa wanajaribu kutumia lugha ya Kiswahili ili kuwa karibu nasi. Mimi nina imani tutafika mbali zaidi.”