Michezo

Hassan Mwakinyo na SportPesa mambo safi, awa bondia wa kwanza kunufaika na udhamini wa kampuni hiyo

Kampuni ya kubashiri michezo ya SportPesa Tanzania leo siku ya Alhamisi ya Oktoba 25, 2018 imepiga hatua nyingine kwenye sekta ya michezo hapa nchini baada ya kumtambulisha bondia Hassan Mwakinyo kama Balozi wa kampuni hiyo. Bondia huyo ambaye kwa sasa ndio anayeongoza katika Ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati katika Uzani wa super welter ameingia katika makubaliano ya miaka mitatu huku akiwakilisha kampuni ya SportPesa Tanzania kwenye matukio yake muhimu.

Bondia Hassan Mwakinyo mnamo Septemba mwaka huu alifanya mambo makubwa baada ya kumchapa Muingereza Sam Eggington kwa Technical Knock Out kwenye raundi ya pili kwenye pambano lililokuwa na raundi 10 la uzani wa super welter ambalo lilifanyika kwenye ukumbi wa Barclayeard Arena kule Birmingham, Uingereza. Ushindi huo ulimfanya kufikisha point 115 na kushika nafasi ya 16 duniani na nafasi ya kwanza Afrika kwa uzani wa super welter.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa kumtangaza bondia huyo kuwa Balozi wa kampuni ya SportPesa Tanzania, Mkurugenzi wa Utawala na Utekelezaji SportPesa Tanzania Tarimba Abbas alisema kuwa kampuni ya SportPesa kudhamini michezo imekuwa ni jambo la kawaida. Kampuni yetu mama ya SportPesa Kenya ambao ilianzishwa 2014 imekuwa ikidhamini michezo mingi kama mpira wa miguu, rugby, mchezo wa ngumi na ligi kubwa duniani.

Mkurugenzi wa Utawala na Utekelezaji SportPesa Tanzania Tarimba Abbas

‘Na kwa sababu hiyo, SportPesa Tanzania kwa sasa inafuata njia hiyo kwa kudhamini michezo ya ngumi hapa nchini. Tulianza na mpira wa miguu na sasa tumeingia kwenye mchezo wa ngumi kwa bondia Hassan Mwakinyo kuwa Balozi wa SportPesa kwa mkataba wa miaka mitatu.

Tunaamini ya kwamba kumdhamini Hassan Mwakinyo kutaleta changamoto mpya na kuwa chachu ya kuibua mabondia wengine na kuongeza ushindani na kujiamini na hasa kwenye mapambano ya kimataifa, alisema Tarimba.

Wakati kampuni ya SportPesa ikiendelea katika hatua mbali mbali za ukuaji, tunataka pia kukua na Mwakinyo na kuleta mwanga mpya kwenye mchezo huu wa ngumi hapa nchini, aliongeza Tarimba.

Bondia huyo mwenye umri wa miaka 23 na mwenye rekodi ya (13-2, 8 K0s) alisema kuwa anajisikia furaha sana kwa kampuni kama SportPesa kutambua kipaji chake na kuweza kumuunga mkono kwa kumpa udhamini wa miaka mitatu ambao ni wa kwanza na wa kipekee na hasa kwenye upande wa mchezo wa ngumi hapa nchini. Hii ni muhimu kwangu kwani itaniongezea hamasa na kunifanya nizidi kujulikana zaidi.

“Imeniongezea kujiamini na nataka niwahidi ya kwamba nitazidi kuongeza bidii ili nizidi kupata mafanikio na mimi binafsi lakini pia kwa nchi yangu ya Tanzania” alisema Mwakinyo.

Kuchanguliwa kuwa Balozi wa kampuni ya SportPesa Tanzania ni ishara nzuri kwangu lakini pia kwa sekta ya mchezo wa ngumi hapa Tanzania. Nachukua fursa hii kutoa pongezi kwa serikali kwa kufanya kazi kwa bidii na hatimaye kuweza kurundisha nidhamu ya mchezo wa ngumi hapa nchini na hatimaye tumeanza kufaidika kwa kupata wadhamini kama SportPesa, aliongeza Mwakinyo.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Vijana, Sanaa na Michezo Harrison Mwakyembe aliwapongeza kampuni ya SportPesa kwa kumchangua Hassan Mwakinyo kuwa balozi wake. “Kwa udhamini huu, inaonyesha ni jinsi gani SportPesa wamejitolea kukuza michezo hapa nchini. Vile vile inaonyesha imani yetu kwenye mchezo wa ngumi. Hii ni hatua njema na naomba makampuni mengine kuiga mfano wa SportPesa.

Waziri wa Habari, Vijana, Sanaa na Michezo Harrison Mwakyembe (katikati)

Waziri Mwakyembe alimpongeza Mwakinyo huku akisema ni mmoja ya mabondia wazuri ambao Tanzania ishawahi kuwa nao. Hata hivyo, Mwakyembe alimtaka Mwakinyo kuheshimu mkataba wa udhamini wake kwani kutamjengea heshima na kupata wadhamini wengine zaidi.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents