‘Hat-Trick’ kumpa ugali Philippe Coutinho, Bayern Munich
Mastaa wa Bayern Munich wameuwomba uongozi wa timu hiyo inayoshiriki ligi ya Bundesliga kumpatia mkataba wa kudumu mchezaji mwenzao, Philippe Coutinho baada ya kuonyesha uwezo mkubwa katika mchezo wao dhidi ya Werder Bremen na kuibuka na ushindi mnono wa jumla ya mabao 6-1 uliyopigwa Jumamosi hii.
Nyota huyo wazamani wa Liverpool, alikuwa moto wa kuotea mbali siku hiyo ambapo alifanikiwa kufunga jumla ya mabao matatu ‘hat-trick’ peke yake kati ya sita (6) waliyoshinda dhidi ya Werder Bremen, hali iliyopelekea wachezaji wenzake kuomba apewe kandarasi ya kudumu.
Coutinho yupo hapo kwa mkopo akitokea Barcelona na tayari ameshajijengea mashabiki wengi nchini Ujerumani. Na kwa sasa wachezaji wenzake wanajaribu kumuombea ili aweze kubaki hapo moja kwa moja.
”Ilikuwa kitu bora sana alichofanya hii leo, tunahitaji aina hii ya mchezaji, hakika nimefurahi sana ameonyesha kile anachoweza kufanya,” amesema Robert Lewandowski
David Alaba pia kwa upande wake amesema kuwa ”Kama umeweza kutizama mchezo wa leo, basi tunapaswa tumnunue, si ndiyo ?.”
Hata hivyo ili uweze kumnunua Mbrazil huyo basi lazima ujiandae na kitita cha pauni milioni 100 kutokana na mkataba wake, na Bayern tayari iliamua kuwekeza fedha zake kwa kinda wa miaka 20 wa Bayer Leverkusen, Kai Havertz.