Habari

Haya ndio mashtaka yaliyowapeleka Papa Msofe na wenzake wanne kortini – Video

Haya ndio mashtaka yaliyowapeleka Papa Msofe na wenzake wanne kortini - Video

Mfanyabiashara maarufu Marijan Msofe (53) alimaarufu kama Papa Msofe, Wakili wa Kujitegemea Mwesigwa Mhingo (36) na wenzao watatu, wamefikishwa mahakamani kwa uhujumu uchumi ikiwamo kuratibu genge la uhalifu na kutakatisha Dola za Marekani 410,000.

Washtakiwa hao walifikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana na kusomewa mashtaka na Wakili wa Serikali Mkuu, Maternus Marandu, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Ladislaus Komanya na Wakili wa Serikali, Glory Mwenda.

Wakili Komanya akiwasomea mashtaka  mbele  ya Hakimu Mkazi Mkuu  Huruma Shaidi, aliwataja washtakiwa kuwa ni Papa Msofe, Mhingo, Wenceslaus Mtui (49), Josephine Haule (38) na Fadhili Mganga (61).

Alidai kuwa katika tarehe tofauti kati ya Desemba 2018 na Septemba, mwaka huu washtakiwa wote kwa pamoja na wenzao ambao hawajakamatwa walifanya mpango wa kuongoza genge la uhalifu.

Katika shtaka la pili, alidai kati ya Desemba 2018 na Septemba, mwaka huu washtakiwa wote, mahali tofauti walitakatisha Dola za Marekani 300,000 (sawa na Sh milioni 690) kutoka kwa Pascal Jean Camille.

Shtaka la tatu, inadaiwa kuwa siku ya tukio la pili, washtakiwa wakiwa na nia ovu, walijipatia kwa njia ya udanganyifu Dola za Marekani 300,000 kutoka kwa Camille baada ya kumdanganya kuwa wangemuuzia kilo 200 za madini aina ya dhahabu na kuyasafirisha kwenda nchini Ureno huku wakijua si kweli.

Upande wa Jamhuri ulidai katika shtaka la nne, tarehe tofauti Desemba 2018 na Septemba, mwaka huu washtakiwa walitakatisha Dola za Marekani 110,000 (Sawa na Sh milioni 253) kutoka kwa John Mahsson wakati wakijua ni zao la uhalifu.

Wakili Komanya alidai katika shtaka la tano, washtakiwa walijipatia Dola za Marekani 110,000 kutoka kwa Mahsson baada ya kumlaghai kwamba wangemuuzia kilo 20 za madini aina ya dhahabu na kuyasafirisha kwenda Ureno huku wakijua si kweli.

Washtakiwa hawakutakiwa kujibu kitu kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.

Upande wa Jamhuri ulidai upelelezi wa kesi haujakamilika na waliomba tarehe nyingine ya kutajwa. Mahakama iliahirisha  kesi hiyo na kupangwa itajwe Desemba 16, na washtakiwa walipelekwa mahabusu.

https://www.instagram.com/p/B5mt8laB7UU/

By Ally Juma.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents