Habari

Helikopta ya Jeshi la Marekani yapigwa risasi na watu wasiojulikana 

Shirika la Ujasusi la Marekani limeanzisha uchunguzi baada ya helikopta ya kijeshi kupigwa risasi ilipokuwa inafanya mazoezi ya kawaida katika jimbo la Virginia.

Mtu mmoja alijeruhiwa katika tukio hilo Jumatatu na helikopta hiyo ikalazimika kutua kwa dharura.

Maafisa wanasema kwamba ndege hiyo ilikuwa inapaa umbali ya takriban futi 1,000 (mita 300) kutoka ardhini wakati ilipopigwa risasi.

Tukio hilo lilitokea mapema Jumatatu mchana kilomita 16 (maili 10) kutoka uwanja wa ndege wa Manassas, kaskazini mwa Virginia.

Helikopta hiyo ilitua kwa dharura katika uwanja wa ndege baada ya kupigwa risasi.

Mfanyakazi wa ndege hiyo aliejeruihiwa alipelekwa hospitali lakini ameruhusiwa kwenda nyumbani. Jeshi la Angani limesema kuwa ndege hiyo ya helikopta aina ya UH-1N Huey imeharibika kiasi.

Helikopta hiyo huwa inasafirisha wanajeshi waandamizi, viongozi wa kiraia pamoja na wageni wengine waheshimiwa, na kushughulikia uhamisho wa wagonjwa wakati wa dharura.

Shirika la Upelelezi la Marekani limesema linashirikiana na mashirika mengine ikiwemo afisi ya jeshi la angani inayoshughulika na uchunguzi maalum kutathmini kile kilichotokea.

Maafisa wamesema kwamba risasi hiyo ilifyatuliwa na mtu aliyekuwa ardhini lakini bado haifahamiki ikiwa ndege hiyo ilipigwa risasi kimaksudi au ilikuwa ajali iliyosababishwa na mtu ambaye alikuwa anafyatua risasi hewani kiholela.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents