Henry Apeta Norway
Mambo yanaonekana kwenda safi baada ya kiungo wa zamani wa Simba, Henry Joseph kuanza kucheza nafasi yake ya zamani kwenye timu yake ya Kongsvinger ya Norway.
Kocha wake ameamua kumuondoa katika nafasi ya beki wa kulia aliyokuwa akimtumia kama kiungo wa ulinzi katika mechi mbili za Ligi ya Norway.
Akizungumza kutoka nchini humo, Henry alisema amefurahi kufikia hatua hiyo ingawa hana uhakika sana kwa kuwa anaweza kurudi tena kama beki wa kulia.
“Awali sikufurahia kucheza kama beki wa kulia, lakini niliona kama changamoto tu. Sasa ninacheza kama namba sita na ninaona ni sehemu hasa ninayoitaka,” alisema Henry.
Kikosi cha Kongsvinger ambacho kimepanda msimu huu, kimeonyesha kujitahidi kumiliki mikiki ya ligi hiyo ingawa bado wanaonekana kutakiwa kuimarisha nguvu zaidi.
Henry anayevaa namba mbili mgongoni, alijiunga na timu hiyo akitokea Simba na kuwa mmoja wa wachezaji wa Msimbazi wanaondelea kupata mafanikio nje ya Tanzania.