Burudani

It’s official: BASATA yaufungia wimbo wa Nay wa Mitego ‘Shika Adabu Yako’

BASATA limetoa makucha yake. Hii ni taarifa yake rasmi iliyotoka Ijumaa hii:

nay new2

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limeufungia rasmi wimbo wa ‘Shika Adabu Yako’ ulioimbwa na Msanii Nay wa Mitego kutokana na ukiukwaji mkubwa wa maadili, kashfa, uchochezi, kudhalilisha watu na kuhatarisha amani na utengamano miongoni mwa wasanii na jamii kwa ujumla.

Sambamba na kuufungia wimbo huo, BASATA litampa karipio kali Msanii huyo na kumwagiza kuacha mara moja kujihusisha kwa namna yoyote na tabia ya kuutangaza wimbo au kuusemea katika vyombo vya habari vinginevyo hatua kali zaidi na za kisheria zitachukuliwa.

Ieleweke kwamba kwa mujibu wa kifungu cha 4 (1) (j) cha sheria ya BASATA namba 23 ya mwaka 1984, Baraza limepwa mamlaka ya kuratibu na kufuatilia mienendo ya mtu yeyote anayehusika na kazi za Sanaa na kuhakikisha linalinda maadili ya kitaifa miongoni mwa Wasanii wanapokuwa jukwaani au wanapobuni kazi yoyote ya Sanaa.

Aidha, kifungu cha 4 (2) cha sheria hii kinalipa Baraza nguvu ya kisheria kufanya jambo lolote lile kuliwezesha kufanya majukumu yake kwa faida na ustawi wataifa.

Baraza la Sanaa la Taifa limekuwa likipokea simu za maswali na malalamiko kadhaa kutoka kwa waandishi wa habari na wadau wa Sanaa ambao kwa njia moja ama nyingine wameguswa na kuchukizwa na kazi hiyo ambayo si tu inadhalilisha tasnia ya Sanaa bali inawafanya watu makini kuanza kuhoji hadhi ya msanii, weledi na taaluma ya Sanaa kwa ujumla.

BASATA mara kadhaa limekuwa likikemea na kuchukua hatua kadhaa dhidi ya tabia hii chafu ambayo ilianza kujitokeza kwenye kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka jana wa 2015. Kukemea huku ni kwa msingi mmoja kwamba asili ya tasnia hii ya Sanaa ni kuelimisha jamii, kukosoa pale kunapokuwa na tatizo, kuburudisha na kujenga jamii yenye staha, umoja wa kitaifa, mshikamano na amani.

Ni wazi wasanii wengi wanafanya kazi zao vizuri, kwa kubuni kazi zenye ubora, zenye kujenga jamii na zaidi zinazoburudisha rika zote kiasi cha kuzifanya zililetee heshima taifa. Kati ya hawa wengi, kuna wachache ambao wanaipaka matope tasnia ya Sanaa na kwa kiasi kikubwa wanaonesha wazi kutokuwa na nia njema.

Kwa mantiki hii BASATA halitavumilia hawa ‘wasanii’ wachache ambao wanataka kuigeuza tasnia ya Sanaa na wasanii genge la wahuni, wasio na staha, wa kudharaulika na waliojipanga kuibomoa jamii na kuharibu amani na utulivu uliopo nchini.

BASATA linapenda kueleza yafuatayo:

1. Vyombo vya habari viwe vya kwanza kuchuja maudhui ya kazi yoyote ya Sanaa kabla ya kuingia kwenye mtego wa kuwa mawakala wa uharibifu wa jamii kupitia kucheza kazi chafu za Sanaa. BASATA lilishaziandikia radio zote kuzishauri kuwa na kamati za maudhui ya kazi za Sanaa lakini inashangaza baadhi ya vyombo vya habari vinakuwa vya kwanza kushabikia nyimbo hizo chafu na kuwapa muda mrefu wa mahojiano wasanii hao na baadaye kurudi BASATA kuhoji uhalali wa nyimbo husika. Hii si sawa hata kidogo.

2. Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli imejipanga kuwajengea mazingira bora ya utendaji Wasanii wote nchini kupitia kuboresha miundombinu ya Sera, Sheria na Kanuni. Hata hivyo, uwepo wa Wasanii kama hawa unafanya jamii kuhoji hadhi ya wasanii, nafasi yao katika jamii na kwa maana hiyo kukatisha tamaa juhudi za kuipa msukumo sekta hii maana wadau wakuu ambao ni wasanii wanaanza kuoneasha kuwa mawakala wa uharibifu wa jamii.

3. BASATA linawataka wasanii kujiuliza mara mbili kabla ya kubuni kazi zao za Sanaa. Wafikirie wazazi, ndugu, jamaa na marafiki zao watazipokeaje? Wavae nafasi ya wale wanaowatukana na kuwadhalilisha, Waelewe kwamba Sanaa si uwanja wa kutusi na kudhalilisha watu hata kidogo. Ikitokea wale wanaotukanwa na kudhalilishwa kughafilika Sanaa itakuwa uwanja wa vita. Hili halikubaliki.

4. Tunafahamu kuna wasanii wamekuwa wakifanya hivyo makusudi kutafuta ‘umaarufu uchwara’ ambao wanadhani utakuja kutokana na kuzungumziwa sana. Tunapenda kusema wazi kwamba umaarufu hauji kwa upuuzi wa namna hiyo unakuja kwa msanii mwenyewe kujiheshimu, kujituma, kubuni kazi bora na zenye kulifahamu vema soko la ndani na la kimataifa.

SANAA NI KAZI TUIKUZE, TUILINDE NA KUITHAMINI

Godfrey L. Mngereza
KATIBU MTENDAJI, BASATA

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents