Habari

Je unajua kuhusu utapeli huu?

Matapeli ni matapeli tu hapa mjini. Siku ya tarehe 8 mwezi wa tisa mwaka huu nilipokea simu kutoka kwa jamaa mmoja aliyejitambulisha kwa jina halafu akinipongeza kwa kufunga ndoa na habari nyingi kedekede ili aweza kurubuni kichwa changu iwe kana kwamba tunafahamiana.

con-man-2

Ilibidi nimsikilize huku akija na ajira anayoifanya na kusema kwamba yeye ni afisa manunuzi wa Dawasco lakini wako kwenye miradi ya kuchimba visima huko Mpwapwa.

Mara akaja na ajenda “eti Bwana Awali tumekuchagua ili uweze kusupply vifaa vya uchimbaji visima ofisini kwetu kwa sababu aliyekuwa anafanya kazi hii hapatikani kwenye simu na baada ya kufuatilia jamaa alisafiri kwenda Ulaya na wala hatarudi hivi karibuni. Hata hivyo tunasafiri muda si mrefu tunatoka Mpwapwa na leo jioni tutakuwa Dar ili tuweze kukamilisha mpango huu.”

Nikajiuliza haraka haraka mimi si mfanyabiashara wa hizo mashine wanazozizungumzia, bila kupoteza muda nikagundua hawa ni matapeli hivyo, nikamwambia, “mimi sio supplier” akazuga “basi ngoja tutafute mtu mwingine.”

Baada ya kugundua hivyo nikaandika kwenye mitandao ya kijamii na ndipo nilipogundua watu wengi wamekuwa wakipigiwa simu na wengi ni wasomi wakubwa tu wamekwisha tapeliwa ila hawawezi kusema yaliyowasibu.  Je ni watu wangapi wanatapeliwa na wamekaa kimya? Je watu wanajua aina hii ya utapeli?

Mtu mmoja anasema hivi; Jamaa yangu walimliza aisee sitasahau na siku hiyo tulikuwa na test chuo mwaka huu huu…aliahirisha akaanza kutafuta gari … na ile Gari wakamwambia inahitaji matengenezo atume laki tano waikarabati…akanipigia nimkopee 250,000 hata kwa riba sawa ili aipate hiyo laki 5 …bwana weeeee aliituma ile hela na baadaye wanunuzi wakamtumia muamala fake tigo pesa…alidata na  ana madeni juu na wala gari mzigo hakupa.”

Mtu mwingine naye anasema: Yaaani hao jamaa hatari sana…waliwahi kuniambia tukaonane airport eti kuna medical delegates wanakuja, wamenichagua niwe representative wao Dar, ila kuna pesa kama 1m inahitajika then watanipa 2m baada ya kubadilisha dola. Nilipowashitukia wakakata simu”..Matapeli wengine Bwana! hivi mnafikiri mnaweza kunipata kirahisi namna hiyo?

Na ni kwanini watu wengi wanatapeliwa? Kwa uchunguzi mdogo ambao matapeli wameshafanya ni kuwa watu wengi tunapenda mafanikio ya fasta fasta na kwasababu hiyo tuko tayari kucheza dili za hapa na pale tupate hela hiyo ya haraka.

Matapeli hao kwa kulijua hilo, wanakupa chambo na ukiingia kwenye mtaro wao wanakula hela yako na kuondoka huku ukijiuliza kumetokea nini? Wengi wametapeliwa kwa ajili ya kutafuta vyuo vya nje na wengine kwa ajili ya kutaka kupewa tenda za kusambaza vifaa kwenye ofisi fulani fulani.

Hakuna pesa ya bure au mafanikio ya bure ambayo yatakukuta hapo hapo, unahitaji kuwa mwangalifu na kuchukua tahadhari. Kuna utapeli mwingi unaendelea hapa mjini na inawezekana umeathirika kwa namna moja ama nyingine si vibaya ukisema ili watu wengine wasiingie kwenye shimo hilo hilo ulilotumbukia. Najua wengi wanaona aibu kusema kwasababu ya elimu zao na nyadhifa zao wataonekanaje kwenye jamii kama na wao wametapeliwa?

Awali Mwaisanila

A Personal Career Development specialist, passionate about empowering emerging generations of student, graduates and working class.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents