Habari

Jeshi la polisi lampotezea bilionea Dkt. Shika, Latoa sababu za kumsamehe

Kamanda Lazaro Mambosasa

Jeshi la Polisi limetangaza kuachana na Bilionea mtata, Dkt. Louis Shika, ambaye alifika bei ya kununua majengo ya mfanyabiashara Said Lugumi.

Akithibitisha taarifa hizo, Kamanda wa polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema kesi waliyomfungulia Dkt. Shika ya kuharibu mnada hawataendelea nayo kwa kuwa nyumba za Lugumi alizoahidi kuzinunua zote zipo na haijatokea hasara yoyote kwenye mnada huo.

Dkt. Shika ni wa kumuonea huruma hana kitu, tulisema tunamchunguza na tutampeleka mahakamani lakini tumeona kesi yake haina mashiko, ndiyo maana hatuendelei nayo.” amesema Mambosasa.

Ikumbukwe mnamo tarehe 9 Novemba 2017, kampuni ya udalali ya Yono kwa niaba ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) iliendesha mnada wa nyumba za Lugumi zilizopo Mbweni JKT na moja Upanga jijini Dar es Salaam ambazo zote Dkt. Shika alifikia bei ya kuzinunua kwa Sh3.2 bilioni.

Dkt. Shika ambaye taaluma yake ni ya udaktari kutoka Urusi alishindwa kulipa asilimia 25, kwa mujibu wa taratibu za minada na hivyo kukamatwa kisha kushikiliwa na jeshi hilo kwa siku kadhaa kabla ya kuachiwa kwa kujidhamini mwenyewe.

Msomi huyo alijizolea umaarufu baada ya kushindwa kulipa asilimia 25 ya fedha alizotakiwa kutoa papo hapo baada ya kufikia dau.

Chanzo:Mwananchi

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents