Kikwete Amshukia Waziri Wa Nishati
Rais Jakaya Kikwete amesema haridhishwi na utendaji kazi wa Wizara ya Nishati na Madini, katika kushughulikia suala la kampuni ya Independent Plant Tanzania Limited (IPTL).
Rais Jakaya Kikwete amesema haridhishwi na utendaji kazi wa Wizara ya Nishati na Madini, katika kushughulikia suala la kampuni ya Independent Plant Tanzania Limited (IPTL).
Alisema wizara hiyo inayoongozwa na waziri wake, William Ngeleja, imeshindwa kubadili mfumo wa mitambo ya IPTL ili itumie gesi ili kupunguza gharama za uzalishaji wa nishati hiyo muhimu kwa maendeleo nchini.
Kwa hali ilivyo sasa, mitambo hiyo inatumia mafuta, hali inayosababisha kuwepo gharama kubwa za uzalishaji wa umeme, ambazo kimsingi zinafidiwa na wateja.
Rais Kikwete, alisema hayo jana wakati akihutubia katika hafla ya uzinduzi wa mtambo wa gesi unaomilikiwa na serikali kupitia Shirika la Umeme (Tanesco), uliopo Ubungo jijini Dar es Salaam.
“Kasi ya kubadilisha mitambo sijaridhika nayo, hekima inabidi itumike ili kuhakikisha kuwa mabadiliko hayo yanafanyika,“ alisema.
Rais Kikwete alisema katika mazungumzo yake na Ngeleja, aliyehudhuria hafla hiyo, alijulishwa kuwa mabadiliko hayo yanasubiri kukamilika kwa mchakato wa kuimilikisha IPTL kwa serikali.
“Uamuzi wa kubadili mfumo wa mitambo ya IPTL hahusiki na suala la umiliki, tunachotaka ni kuona mitambo hiyo inabadilishwa,“ alisisitiza.
Rais Kikwete, alitoa mfano kuwa, alipokuwa Waziri wa Nishati na Madini, alifanikisha kubadilisha mitambo ya Songas kutoka mafuta kutumia gesi, hali iliyosababisha kushuka kwa gharama za uzalishaji kutoka Sh milioni 5 kufikia Sh milioni moja.