Kilimanjaro Stars Yatakata, Yaanza Vyema Cecafa Tusker Challenge Cup
Alikuwa ni Staika wa kutumainiwa wa timu ya Azam FC, John Bocco aliyefunga bao la kwanza akiiwahi vema krosi ya Ngassa aliyewatoka mabeki wa Sudan, kutokea wingi ya kushoto na kuitumbukiza kimiani dakika ya 14 tangu kuanza kwa kipindi cha kwanza.
Alikuwa ni Adebayor tena, ambaye aliwainua vitini mashabiki wa Tanzania, katika dakika ya 28 ya kipindi cha kwanza, akiunganisha krosi ya Mrisho Ngassa ambaye alitumia upande ule ule tena akitokea upande wa kushoto mwa uwanja wa Namboole.
Kwa ujumla Tanzania Bara walicheza vizuri kipindi cha kwanza, wakishambulia zaidi kupitia pembeni, wakitumia vyema mawinga wa upande wa kulia Simon Msuva ambaye hakuwa na madhara sana na upande wa kushoto akitumika Mrisho Ngassa ambaye alikuwa mwiba mchungu haswa kwa Wasudan.
Timu ya Kilimanjaro Stars ilicheza vizuri katika kipindi cha kwanza, na kupotea kidogo kipindi cha pili na kuwapa Wasudan mwanya wa kufanya mashambulizi ya kushitukiza, ambayo yalidhibitiwa kwa uhakika na mlinda mlango Juma Kaseja, ambaye aliokoa michomo kadha wa kadha na kuliweka lango lake salama.
Michuano hiyo ilianza rasmi siku ya jana kwa mchezo mmoja wa ufunguzi, ambao ulihusisha timu za kundi A, ambapo timu ya taifa ya Uganda ilipambana na timu ya taifa ya Kenya na kushinda kwa goli moja kwa bila.
Michuano hiyo itaendelea siku ya kesho ambapo timu za kundi C zitakapopambana.
Picha kwa hisani ya bongostaz.blogspot.com