Habari

Kim Jong Un adai nchi yake imefanikiwa dhidi ya janga la Corona

Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un ameisifu nchi yake kwa kile alichokitaja kuwa imepata “mafanikio ya kung’ara” katika kukabiliana Covid-19, kwa mujibu wa shirika la habari la taifa hilo – KCNA.

North Korean leader Kim Jong Un is seen providing over a meeting on Thursday in this photograph supplied by KCNA.

Akizungumza katika mkutano wa kamati kuu ya watunga sera wa Chama tawala cha kikomunisti -politburo, Bwana Kim alisema kuwa nchi hiyo “ilizuia kusambaa kwa virusi hatari na kuimarisha hali “.

Korea Kaskazini ilifunga mipaka yake na kuwaweka maelfu ya watu katika karantini miezi iliyopita wakati virusi viliposambaa duniani.

Ilidai kuwa haikua na virusi vya corona, ingawa wachambuzi wanasema huenda isiwe sahihi.

Bwana Kim anasemekana kuwa “alitathimini kwa kina miezi sita ya kukabiliana na janga” katika mkutano wa politburo siku ya Alhamisi. Alisema kuwa mafanikio katika kushughulikia virusi ” yalifikiwa kutokana na uongozi unaoona mbali wa Kamati Kuu ya Chama”.

Lakini alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ” tahadhari ya hali ya juu bila … kulegeza mapambano dhidi ya janga “, akiongeza kuwa virusi bado vipo katika mataifa jirani.

“Alirejelea onyo kwamba kulegezwa kwa hatua za kupambana na janga la corona kutasababisha mzozo usiofikirika na ambao hauwezi kutatuliwa ,” ripoti ya KCNA ilisema Ijumaa.Korea Kaskazini

Je virusi vya corona vilisambaa Korea Kaskazini?… Hakuna mtu yeyote anayejua hilo. Nchi imefungwa tangu Januari 30. Ni watu wachache sana walioweza kutoka ndani ya nchi.

Shirikisho la kimataifa la msalaba mwekundu lina wahudumu wa kujitolea katika eneo la mpakani wanaotoa huduma ya hatua za kuzuia maambukizi ya virusi na kumekuwa na ripoti kadhaa ambazo hazijathibitishwa za watu wenye virusi ndani ya nchi hiyo.

Lakini taarifa nyingi kuhusu maisha katika mji mkuu zilizotolewa katika wiki za hivi karibuni zinaonekana kuonesha kuwa maisha yanaendelea kama kawaida

Kwa hali yoyote ile, Pyongyang inataka kuonekana kuwa kweli imemaliza ugonjwa wa Covid-19.

Ndani ya nchi huu ni ujumbe thabiti kwamba hatua kali ambazo Bwana Kim Jong-un alichukua kukabiliana na virusi zimefanikiwa

Huku maeneo mengine ya dunia yakiendelea kuathiriwa na virusi , Bwana Kim anataka watu wake wajue kuwa amewaokoa na janga hilo.

Lakini hilo limekuja na gharama. Ushuru wote wa mpaka umepunguzwa. Hiyo ina maana kwamba kuingiza bidhaa muhimu katika taifa hilo limekua ni jambo lisilowezekana.

Duru za kidiplomasia zimeniambia kuwa kuna marundo ya vifaa vya kujikinga na maambukizi -PPE na za matibabu, zikiwemo chanjo ambazo zimekwama katika mpaka ambazo hazikuweza kupita.

Kulikuwa na taarifa kadhaa za watu kununua bidhaa za kimataifa kwa pupa katika maduka makubwa ya mjini Pyongyang. Maduka yaliachwa wazi kutokana na masharti yaliyowekwa kuhusu uzalishaji wa bidhaa.

Pia ni muhimu kutambua kuwa ni watu 12 pekee walioweza kufanikiwa kutoroka nchi hiyo na kuingia Korea Kusini kati ya mwezi Aprili na Juni mwaka huu – Ikiwa ni idadi ya chini zaidi kuwahi kurekodiwa.

Watu wa Korea Kaskazini huenda hawaumizwi na virusi vya corona, lakini sasa wametengwa na maeneo megine ya dunia.

Barakoa ni za lazima Korea Kaskazini.

Mwishoni mwa mwezi Januari, Korea Kaskazini ilichukua hatua za haraka dhidi ya virusi kwa kufunga mipaka yake na baadaye kuwaweka katika karantini mamia ya wageni katika mji mkuu, Pyongyang.

Pia iliwatenga maelfu ya raia wake na kufunga shule.Kuvaa barakoa ni lazima katika maeneo ya umma Korea Kaskazini

Korea Kaskazini sasa imefungua shule, lakini imeendelea kutekeleza marufuku ya mikusanyiko ya Umma na imeweka amri ya watu kuvaa barakoa katika maeneo ya Umma, ilisema ripoti ya Reuters ya tarehe 1 Julai ikimnukuu afisa wa Shirika la Afya duniani.

WHO pia iliripoti kuwa nchi hiyo imewapima virusi watu 922 ambao wote hawakupatikana na virusi.

Korea Kaskazini, ambayo inapakana na China, kwa muda mrefu imekuwa ikisema kuwa hakuna mtu hata mmoja aliyewahi kupata maambukizi ya virusi vya corona nchini humo.

Hatahivyo, Oliver Hotham, mhariri mkuu wa mtandao wa habari wa taarifa za kitaalamu NK News, aliiambia BBC mapema mwaka huu kwamba hilo huenda lisiwe kweli.

“Huenda isiwe hivyo kabisa kwamba hakuna maambukizi ya corona kwasababu inapakana na China na Korea Kusini . [Hasa na China], ikizingatiwa biashara za mpakani zinazoendelea… Kusema ukweli sioni ni vipi walivyoweza kuizuia,” alisema.

”Lakini,kusema kweli walichukua tahadhari mapema, kwahiyo inawezekana wamezuia mlipuko kamili .”

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents