Kipre Tchetche apata kibali cha kucheza soka katika klabu ya Al Suwaiq FC ya Oman
Mshambuliaji wa zamani wa klabu ya Azam Fc, Kipre Herman Tchetche hatimaye amepata kibali cha kucheza soka katika klabu ya Al Suwaiq FC ya Ligi Kuu ya Oman kwa dola za Kimarekani 50, 000 zaidi ya Sh. Milioni 100 za Tanzania.
Hatua hiyo imemfanya Tchetche, raia wa Ivory Coast aondoke klabu ya Al-Nahda Al-Buraimi pia ya Ligi Kuu ya Oman, ambayo ndiyo ilimtoa Azam FC akiwa amebakiza Mkataba wa mwaka mmoja.
Licha ya Al Nahda kumalizana na Kipre Tchetche, lakini kwa kushindwa kulipa dola 50,000 za kuvunja Mkataba wa mchezaji huyo na Azam FC imemkosa.
Akizungumza na mtandao wa Bin Zubeiry kutoka Oman, Kipre alisema kwamba amejiunga na Suwaiq ambayo imelipa fedha za kuvunja Mkataba wa Azam FC na tayari Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limetoa Hati yake ya Uhamisho wake wa Kimataifa (ITC).
Na amesema tayari amepata Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC), ambayo sasa inamfanya aanze kucheza Ligi ya Oman.
“Kwa sasa nipo klabu ya Suwaiq FC, baada ya Al Nahda kushindwa kulipa fedha za Azam,”amesema.
Source: Bin Zubeiry