Michezo

Kocha mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera asema ‘Hao Township Rollers mbona tunawapiga tu, nimeandaa fomesheni zaidi ya tatu za kuwavuruga’

Kocha mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera asema 'Hao Township Rollers mbona tunawapiga tu, nimeandaa fomesheni zaidi ya tatu za kuwavuruga'

Kocha mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera, amesema kikosi chake kitapambana kupata ushindi katika mchezo wa marudiano Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Township Rollers ya Botswana utakaochezwa kesho jijini Gaborone. Timu hizo zilipokutana katika mchezo wa kwanza uliyochezwa Agosti 10 mwaka huu, Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Yanga ililazimishwa sare ya bao 1-1. Mchezo huo wa marudiano utakuwa mgumu zaidi hususan kwa Yanga kutokana na faida waliyoipata wapinzani wao, Rollers baada ya kufunga bao la ugenini.

Yanga inahitaji ushindi wowote au sare ya kuanzia mabao mawili ili kutinga raundi ya kwanza ya michuano hiyo. Akifahamu uzito wa kazi iliyo mbele yao, Zahera ameahidi kuwa kikosi chake kitaibuka na ushindi katika mchezo huo kutokana na maandalizi mazuri waliyoyafanya kuelekea mchezo huo. Alisema kambi ya siku chache waliyoiweka nchini Afrika Kusini ilikuwa mahususi kwa ajili ya kusuka mikakati ya mwisho mwisho ya ushindi kabla ya kushuka dimbani kesho.

“Tumejiandaa vizuri kwa mchezo huo, kila mchezaji yuko fiti sina kikubwa cha kuwaambia mashabiki wetu, lakini watarajie ushindi mnono tofauti na mechi zingine zilizopita. “Katika michezo yetu yote ambayo tumecheza na timu za kimataifa, hakuna ambayo tumepoteza hivyo hakuna haja ya kuhofia, wachezaji wamepania kucheza kufa na kupona kuhakikisha timu inaibuka ushindi ili kusonga mbele katika michuano hiyo,” alisema.

Zahera aliongeza ameandaa fomesheni zaidi ya tatu ambazo ana uhakika zitawalaza hoi Rollers mbele ya mashabiki wao 22,500 watakaojitokeza kushuhudia mpambano huo kulingana na uwezo wa uwanja huo. “Nina wachezaji wengi sana wazuri kwenye kikosi changu, hilo linanipa nafasi ya kufanya machaguo mbalimbali, lakini katika mchezo huu, nitachezesha fomesheni zaidi ya moja ili kuwavuruga wapinzani wetu. “Tunahitaji kushambulia mwanzo mwisho kwenye mchezo huo, hivyo lazima tuwe na mbinu zaidi ya moja ili kupata ushindi, najua wanawajua baadhi ya wachezaji wetu tishio, nimeandaa wengine na kuwapa majukumu kuhakikisha ushindi unapatikana kwenye mchezo huo,” alisema Zahera.

Timu hizi mbili zilikutana mara ya mwisho mwaka jana kufuzu hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo Yanga ilitolewa kwa jumla ya mabao 2-1 na mabingwa hao wa Botswana. Yanga ilianza kwa kukubali kichapo cha mabao 2-1 nyumbani, kabla ya kulazimishwa sare ya kutofungana katika mchezo wa marudiano uliochezwa ugenini.

Chanzo Mtanzania digital.

By Ally Juma.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents