Lionel Messi ashutumiwa kulipwa tshs bilioni 7.9 kwa kuweka jiwe la msingi kwenye uwanja wa mpira nchini Gabon
Mshambuliaji wa Barcelona, Lionel Messi anadaiwa kupokea pound milioni 2.4 cash (sawa na shilingi 7,946,003,343), kutoka kwa Rais wa Gabon, Ali Bongo kama malipo ya kwenda kuweka jiwe la msingi kwenye uwanja wa mpira.
Mchezaji huyo aliwasili nchini humo akiwa amevalia t-shirt na kaptura ya jeans na kuweka jiwe la msingi kwenye uwanja mpya wa mpira uliopo kwenye mji wa Port-Gentil.
Mshambuliaji huyo wa Argentina pia alikuwepo kwenye uzinduzi wa mgahawa mpya wa familia ya rais Bongo anayedaiwa kuwa fisadi mkubwa.
Vyombo vya habari vya Ufaransa vimeripoti kuwa mchezaji huyo alipokea fedha hizo pamoja na mchezaji mwenzake wa Barcelona, Deco.
Polisi nchini Ufaransa wamekuwa wakichunguza mara nyingi madai ya rushwa dhidi ya familia ya Bongo ambayo inadaiwa kuwa na nyumba za kifahari 39 zikiwemo za Paris.
Ali Bongo Ondimba, anadaiwa kutumia fedha za umma kwa matumizi yake binafsi na amekuwa akiendelea kushikilia madaraka kwa kipindi kirefu.
Mwaka 1999 alidaiwa kuweka fedha kiasi cha dola milioni 130 kwenye akaunti yake binafsi ya Citibank.
Chanzo: Daily Mail