Bongo5 Makala

Makala: ‘Tupogo’ ya Ommy Dimpoz inatengeneza ‘Kanuni Mpya’ kwenye Bongo Flava

Unawezaje kuwashawishi watu walitumie jina la wimbo wako kwenye mazungumzo ya kawaida? Imenitokea zaidi ya mara tatu pale ambapo nikitoa salamu kwa wenzangu hapa Bongo5. ‘Aisee sisi tupogo tu,’ ni jibu lililoanza kuwa maarufu kwa muda mfupi.

Attachment-1

Thanks kwa Omari Faraja Nyembo ambaye alimelipa nguvu neno hili ambalo kwa wakati mwingine huenda umeshawahi kulisikia kwa mtu akilitumia kwa aina nyingine, kwa mfano ‘Naendako’.

Ni aina ya uongeaji ambao wakazi wa Mwanza na mikoa mingine nchini huyatumia kwenye mazungumzo yao. Hata hivyo Ommy Dimpoz ameliongezea maana zaidi neno hili.

“Tupogo ni jina jipya naweza kusema au msemo mpya kabisa mjini ambao ni tupo na tuna go,” anasema. “Kwahiyo unaweza ukawa na maana moja ama mbili tofauti kwa maana kuna kuna ‘tupo’ na ‘tunago’ katika hali ya mapenzi, mtu na mpenzi wake kwa maana labda mengi yashasemwa lakini nyie mtaongea sisi tupo na tutaendelea kuwepo.”

Mimi ni miongoni mwa watu waliosikia wimbo huu hata kabla haujaachiwa rasmi wiki hii. Niliupenda tu mara ya kwanza nilipousikia hasa kwakuwa nilimsikia Ommy akiwa amekua, amepevuka na mwenye shauku kubwa ya kupiga hatua 100 mbele ya pale Me and You ilipomfikisha. Tupogo inamuonesha Ommy kama mwanamuziki aliyekua haswaa.

Pengine ile background ya kufanya kazi kwenye bendi (Top Band) kwa miaka kadhaa, imemtengeneza kuwa tu si muimbaji wa Bongo Flava, bali wa nyimbo mbalimbali za Kiafrika.

Ommy ana historia ya kuchanganya ladha ya Naija kwenye nyimbo zake lakini kwenye Tupogo amejaribu kutengeneza kitu kikubwa zaidi.

“Nimejaribu kufanya utafiti, unajua wakati mimi mwanzo nilivyoanza kutoa kazi zangu hizi, nilikuwa nimechanganya mahadhi ya West Africa kwa kuchanganya na Bongo Flava fulani hivi. Ukisikiliza muziki wa Tupogo, nimejaribu kuweka kitu fulani more African, kuna Utanzania, yaani muziki fulani mpya katika industry ya Bongo Flava,”anasisitiza.

Tupogo ni wimbo uliochanganya ladha nyingi zikiwemo Jazz hasa pale inapoanza kwa milio ya saxophone. Ina ladha za Kikongo kwa kiasi, Naija kidogo na kuchanganya ladha yenye Utanzania inayoongezewa chumvi na lugha tamu ya Kiswahili.

Wazo la kumshirikisha J.Martins wa Nigeria limepata nguvu zaidi kutokana na mdundo mkali uliotayarishwa kwa ushirikiano wa Man Walter na Marco Chali kutengenezwa kwa ladha yenye Uafrika na unaosikika live.
Imekuwa rahisi kwa J.Martins kutambaa vyema kwenye wimbo huu.

Na wakati msanii na producer huyo wa Nigeria akiianza kuimba, unaweza ukahisi ni Fally Ipupa hasa kwakuwa ameingia na sauti zenye Ulingala fulani.

Tupogo ni miongoni mwa zile nyimbo ambazo mtu wa rika lolote anaweza kuufurahia. Ni wimbo wenye maisha marefu na ambao unaweza kumtambulisha Ommy kwa mashabiki wapya hasa katika nchi tofauti na za Afrika Mashariki ambako jina lake limeenea tayari.

Ni wimbo mtamu na wa kipekee. Umetoka katika kipindi ambacho wasanii wengi wa Tanzania wameachia nyimbo zao. Tupogo unaweza ‘kustand out’ kutokana na upekee huo.

Tupogo umepokelewa vizuri na watu wa aina mbalimbali, wakiwemo wasanii wenzie.

“Nilidhani sipendi mabolingo,kumbe ni sababu kijana wangu Poz Kwa Poz alikuwa hajayafanya…hana kawaida ya kuniangusha…4 songs,zote #1…Mungu akuweke young fella…bonge moja la shipa,TUPOOOGOOOO,” aliandika Mwana FA kwenye Instagram.

Umemgusa pia msanii wa Hip Hop, Nay wa Mitego aliyeandika, “Bonge la ngoma, bonge la kolabo,,, wimbo mkali sanaaaaaa,,, tusupport muziki mzuri. Big up to you broda Ommy Dimpoz hujawahi kosea keep it up.”

Naye Weme Sepetu aliandika: Tupogo…. damn this song… I just loooove this one… Ommy Dimpoz u kip getting beta n beta …. u jus made another hit ryt dea…. no doubt.”

Imewakuna pia maofisa kwenye makampuni makubwa Tanzania akiwemo Operations Manager wa Multichoice Tanzania Ronald B. Shelukindo ‏aliyeandika: This Tupogo tune is very different! Midomo ya bata na magitaa kwa wingii. Umetisha saana mkali. Another classic.”

Naye Mwamvita Makamba wa Vodacom aliandika: Thanks @ommydimpoz for sharing with me your new single TUPOGO – wow I love it! Massive hit- Congratulations – keep at it. Super proud.”

Watu wengine mashuhuri waliompongeza Ommy kwa kazi hiyo ni pamoja na AY, Loveness Diva, Fundi Frank wa Kenya na wengine kibao. Bila shaka kwa Tupogo, Ommy Dimpoz ametengeneza ‘kanuni mpya’ kwenye muziki wa Bongo Flava. Massive Hit.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents