Habari

Makamishna wastaafu polisi watakiwa kuwadhibiti wahalifu uraiani

Makamishna wastaafu wa Polisi Paul Chagonja, Hamdan Omar Makame na Kenneth Kaseke wametakiwa kuendeleza elimu ya Polisi jamii pamoja na kutoa msaada wowote utakaohitajika kwa Jeshi la Polisi pindi wanapokuwa katika maisha ya uraia baada ya kustaafu utumishi wa Jeshi la Polisi ili kuhakikisha kuwa wahalifu hawapati nafasi ya kutamba hapa nchini.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Simon Sirro wakati wa sherehe zilizoambatana na Gwaride maalumu la kuwaaga wastaafu hao lililofanyika katika viwanja vya Chuo cha Maafisa wa Polisi Dar Es Salaam ambapo wastaafu hao walisukumwa kwenye gari maalumu na Makamishna Wasaidizi Waandamizi sita ikiwa ni utaratibu wa Jeshi hilo katika kuwaaga maofisa wakuu.

IGP Sirro alisema kazi waliyofanya wastaafu hao ni kubwa lakini kustaafu kwao siyo mwisho wa kutumika katika kazi za Polisi na hivyo waendelee kuwa tayari wakati wowote kwa kuwa sasa Jeshi la Polisi linaendelea kushirikisha jamii kukabiliana na uhalifu.

“Upolisi ni taaluma kama zilivyo taaluma nyingine hivyo utaalamu hauzeeki na kwetu sisi tunaondelea kubaki Jeshini tutaendelea kufuata yale yote mazuri mliyofanya na nyie mnapokuwa nje ya utumishi endeleeni kutusaidia kwa mawazo na milango yetu ipo wazi ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama” Alisema IGP Sirro

Akizungumza baada ya kuagwa rasmi Jeshini Kamishna Paul Chagonja ambaye alikuwa Kamishna wa Oparesheni na mafunzo kwa muda mrefu amewaasa Maofisa na Askari kuendeleza tamaduni na maadili ya Polisi pamoja na kufanya kazi kwa weledi.

Chagonja amesema nidhamu ndio msingi wa Askari Polisi popote pale wafanyapo kazi zao hivyo amewaomba kuendelea kusimamia sheria bila ya kumuonea muhali mhalifu yeyote.

Kwa upande wake Aliyekuwa Kamishna wa Polisi Zanzibar Hamdan Omar Makame amewashukuru wananchi wote hususani wa Visiwani kwa ushirikiano waliompatia kipindi chote hali ambayo imesababisha Zanzibar kuendelea kuwa shwari.

Sherehe hizo zimehudhuriwa na Viongozi mbalimbali kutoka vyombo vya ulinzi na usalama, Mkurugenzi wa Takukuru Kamishna Valentino Mlowola, IGP Mstaafu Said Mwema, DCI Mstaafu Robert Manumba na Kamishna Mstaafu wa Kanda Maalumu ya Dar Es Salaam Suleiman Kova pamoja na maofisa na Askari Polisi.

Na Jeshi la polisi

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents