Makosa ya herufi yagunduliwa katika mamilioni ya noti Australia, neno ‘responsibility’ lakosewa na kuzua taharuki
Noti mpya nchini Australia ya dola 50 imechapishwa ikiwa na makosa ya herufi, ambayo inatazamwa kuwa aibu.
Benki ya akiba ya Australia (RBA) imeandika neno “responsibility” yaani jukumu au wajibu hivi – “responsibilty” – katika mamilioni ya noti hizo mpya za rangi ya njano.
Imethibitisha kosa hilo la herufi leo na kueleza kwamba litasahihishwa katika noti zitakazochapishwa katika siku zijazo.
Lakini kwa sasa, takriban noti milioni 46 zinatumika nchini.
Zilichapishwa mwishoni mwa mwaka jana na zinamuonyesha Edith Cowan, mbunge wa kwanza mwanamke nchini Australia.
Kinachoonekana kama nyasi nyuma ya bega la Bi Cowan, ni maandishi madogo mno – ya nukuu ya hotuba yake ya kwanza bungeni.
https://www.instagram.com/p/BxN4PpbBRHj/?utm_source=ig_embed
“Ni jukumu kubwa kuwa mwanamke wa kipekee hapa, na nataka nisisitize haja iliopo kwa wanawake wengine kuwepo hapa,” ni maneno yalioandikwa na kuregelewa mara kadhaa kwa hati ndogo mno katika noti hiyo.
Na neno jukumu kwa kizungu ‘responsibility’, limechapishwa mara zote bila ya herufi ‘i’ – na kuandikwa “responsibilty”.
Imechukua zaidi ya miezi 6 kutambua makosa hayo ya herufi.
Noti hiyo ya $50 ndiyo inayotumika sana Australia, na imesambaa pakubwa.
Wakati noti hiyo mpya ilipochapishwa mnamo Oktoba, iliundwa kwa vigezo vya kiusalama kuzuia kuighushi.
Na kama basi unajiuliza iwapo noti hiyo inatumika – ndio, noti hiyo yenye makosa ya herufi inatumika kama sarafu ya nchini humo.