Habari

Mchumba wa Jamal Khashoggi amshtaki mwanamfalme wa Saudia Mohammed Bin Salman kwa mauaji ya mwandishi huyo (+Video)

Mchumba wa mwandishi wa Saudia Jamal Khashoggi aliyeuawa nchini Uturuki amewasilisha kesi mahakamani dhidi ya mwanamfalme wa Saudia, akimtuhumu kwa kuagiza mauaji hayo.

Hatice Cengiz na makundi ya wanaharakati ya haki za kibinadamu yalioanzishwa na Khashoggi kabla ya kifo chake yanamshtaki mwanamfalme Mohammed bin Salman na zaidi ya watu wengine 20 kwa kiwango cha uharibifu kisichojulikana.

Khashoggi aliuawa na kundi la mawakala wa Saudia wakati wa ziara yake katika ubalozi wa Saudia mjini Instabul, Uturuki 2018.

Mwanamfalme huyo amekana kutekeleza mauaji hayo.

Khashoggi alikuwa mkosoaji mkubwa wa serikali ya Saudia na alikuwa akiishi mafichoni nchini Marekani, mara kwa mara akiliandikia gazeti la The Washington Post.

Katika kesi hiyo iliowasilishwa mjini Washington siku ya Jumanne, raia wa Uturuki bi Cengiz anadai kuathiriwa binafsi na kifedha kufuatia kifo cha Khashoggi.

Kundi la kupigania haki za kibinadamu la, Democracy for the Arab World Now (Dawn), linasema kwamba operesheni zake ziliathirika.

Kuuawa kwa Jamal Khashoggi kulisababisha ghadhabu ulimwenguni

Mashtaka hayo yanadai kwamba Khashoggi aliuawa ”kufuatia maagizo kutoka kwa mshukiwa Mohammed bin Salman”.

“Lengo jingine la mauaji hayo lilikuwa wazi – Kumzuia bwana Khashoggi kupigania mabadiliko ya kidemokrasia katika ulimwengu wa Waarabu akiwa nchini Marekani”, ilisema kesi hiyo.

Katika mkutano uliofanyika kupitia video siku ya Jumanne, mawakili wa bi Cengiz na Dawn walisema kwamba lengo la kesi hiyo ni kuilazimu mahakama ya Marekani kumwajibisha mwanamfalme huyo kwa mauaji hayo na kupata stakhabadhi zinazoonesha ukweli, kulingana na gazeti la The Washington Post.

”Jamal aliamnini kwamba kila kitu kinawezekana Marekani na sasa naweka imani yangu chini ya mfumo wa mahakama ili kupata haki na uwajibikaji”, bi Cengizi alisema katika taarifa yake.

Je Jamal Khashoggi ni nani?

Jamal Khashoggi ni mwandishi maarufu aliyeangazia taarifa kubwa kwa mashirika tofauti nchini Saudia.

Aliunda urafiki na Osama bin Laden katika miaka yake ya kwanza alipoanza kuwa mwandishi habari na alifahamika kama mzaliwa maarufu wa Saudia aliyelazimika kutoroka nchi hiyo.

Kabla ya kutoweka kwake katika ubalozi wa Saudia mjini Istanbul, uhamisho wa kibinfasi wa Khashoggi ulimlazimu kuishi baina ya Marekani, Uingereza na Uturuki.

Aliondoka Saudi Arabia mnamo Septemba 2017, baada ya kukosana na maafisa katika ufalme wa nchi hiyo.

Akiwa uhamishoni, alikuwa akiandikia gazeti la Washington Post Marekani nakala kali za kuukosoa utawala wa Saudia, na pia katika akunti yake ya Twitter ambako alikuwa na wafuasi zaidi ya milioni 1.6.

Mwanamfalme Mohammed bin Salman amekosolewa kuhusiana na kuuawa kwa mwanahabari Jamal Khashoggi

Je Jamal Khashoggi aliuawa vipi?

Alionekana mara ya mwisho akiingia ubalozi wa Saudia tarehe 2 Oktoba 2018 ili kuchukua stakhabadhi alizohitaji ili kumuoa bi Cengiz.

Baada ya kusikiliza sauti zilizorekodiwa kuhusu mazungumzo yaliokuwa yakiendelea katika ubalozi huo, yaliopatikana na maafisa wa ujasusi wa Uturuki , Mtaalam maalum wa Umoja wa Mataifa Agnes Callamard alihitimisha kwamba Khashoggi aliuawa kikatili siku hiyo.

Idara ya kuendesha mashtaka nchini Saudia ilisema kwamba mauaji hayo hayakupangwa.

Ilisema kwamba mauaji hayo yaliagizwa na mkuu wa kundi la wazungumzaji waliotumwa mjini Istanbul kumrudisha Khashoggi Saudia kwa njia ya kumbembeleza ama iwapo hilo litafeli kwa lazima.

Mwandishi huyo alikamatwa kwa lazima baada kukataa kufuata maagizo na kudungwa sindano iliokuwa na dawa nyingi, hatua ilionmfanya kulala na kuuawa, kulingana na waendesha mashtaka wa Saudia.

Mwili wake baadaye ulikatwakatwa na kupatiwa mshiriki mmoja nchini Uturuki nje ya ubalozi.

Mawili wake hayakupatikana.

Waendesha mashtaka wa Uturuki walihitimisha kwamba Khashoggi alizuiwa kupumua muda tu alipoingia katika ubalozi huo na kwamba mwili wake uliharibiwa.

Mnamo mwezi Disemba 2019, Mahakama ya uhalifu ya Riyadh iliwahukumu watu watano kifo kwa kutekeleza moja kwa moja mauaji ya mwathiriwa.

Watu wengine watatu walikabidhiwa hukumu za kifungo jela cha miaka 24 kwa kuficha uhalifu huo na kukiuka sheria.

Watu watatu walipatikana na hatia, aliyekuwa naibu wa kitengo cha Ujasusi nchini Saudia Ahmad Asiri.

Saud al-Qahtani, aliyekuwa mshauri mkuu wa mwanamfalme Mohammed , alichunguzwa na kitengo cha mashatka cha Saudia lakini hakushtakiwa.

Mwezi uliopita, vyombo vya habari vya serikali viliripoti kwamba hukumu hiyo ya miaka 24 iliopatiwa washukiwa watano ilipunguzwa na kuwa miaka 20 jela.

https://www.instagram.com/p/CGopNYmhE5O/

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents