Mdogo wa JK asikitishwa na tapeli…
Mdogo wa Rais Jakaya Kikwete, Bw. Yusuf Kikwete, amekilalamikia kitendo cha kijana anayetumia jina lake kujipatia mali na kushauri kuwa, watu wa namna hiyo, wanastaili kunyongwa
Na Zainab Kihate, PST Bagamoyo
Mdogo wa Rais Jakaya Kikwete, Bw. Yusuf Kikwete, amekilalamikia kitendo cha kijana anayetumia jina lake kujipatia mali na kushauri kuwa, watu wa namna hiyo, wanastaili kunyongwa.
Mtu mmoja aliyetambulisho kwa jina la Yusuf Kikwete, alitiwa mbaroni wiki iliyopita kwa tuhuma za kutumia jina hilo kuwatapeli watu mbalimbali kujipatia fedha.
Akizungumza na PST mwishoni mwa wiki, mdogo halali wa Rais Kikwete, Bw. Yusuf alisema amekerwa mno na tabia ya mtu huyo na anashindwa kuelewa lengo lake kubwa lilikuwa ni nini.
Yusuph alisema kwa kipindi kirefu kijana huyo, ambaye jina lake halisi ni Paul Mkondo, amekuwa akitumia jina la Yusuf na kujipatia fedha kutoka kwa watu mbalimbali.
“Watu kama hawa hawafai katika jamii, wanapaswa kunyongwa kwa mtu wa kawaida ni vigumu kutumia jina la mwenzake kwa lengo la kujipatia fedha,“ alisema.
Alisema mwaka 2005, alikwenda kutoa ushahidi katika Mahakama ya Morogoro kufuatia kijana huyo kutumia jina hilo hilo la Yusuf na alihukumiwa kifungo cha miaka miwili jela kwa kosa hilo.
Hata hivyo, kwa mujibu wa Bw. Yusuf, mshtakiwa huyo alitolewa kwa msamaha wa Rais.
“Nilifikiri pengine atajirekebisha baada ya kukaa gerezani, kumbe ndio kwanza amepata uzoefu mkubwa zaidi wa kutapeli watu,“ alisema Bw. Yusuf.
Alisema mara kwa mara, alikuwa akipata usumbufu baada ya watu anaowatapeli kufikisha malalamiko yao ngazi za juu na hatimaye kuitwa yeye kwa ajili ya kumtambua.
Hata hivyo, Bw. Yusuf alikiri kumtambua kijana huyo na kudai kuwa, wanatoka kijiji kimoja cha Msoga, wilayani Bagamoyo.
Source: Nipashe