Burudani

Mfahamu kiundani msanii aliyeimba Sikomi ya Diamond kwenye The Voice Afrique

Asubuhi kumekucha na makucha yake! Natafuta simu yangu kuweza kufahamu ni habari gani zinaendelea nchini huku pia nikitafuta ubuyu mpya maana kwenye hilo Watanzania tayari tumeshatunukiwa PHD kwenye upande huo – Hahahaha! Natania tu.

Wakati nikiperuzi nikakutana na clip nyingi zikimuonyesha kijana mmoja ambaye anaonekana siyo Mtanzania lakini akiimba wimbo wa ‘Sikomi’ wa Diamond kwenye tamasha moja kubwa la kusaka vipaji linalofahamika kama The Voice Afrique 2018.

Nilitaka kumfahamu kijana huyo ilipia niweze kuwafahamisha japo kwa kidogo kuhusu kijana huyo. Kwa jitihada za Bongo5 tunakuja kukufahamisha kijana huyo ambaye ameteka vichwa vingi vya habari kutokana na video hiyo huku tukiona muziki wetu wa Bongo Flava unazidi kupenya.

Kijana huyo anatumia jina la Dadiposlim na anatokea kwenye mji wa Moroni ulipo katika nchi ya Comoro.

Lakini katika harakati za muziki wake Dadiposlim, Januari 26 aliachia albamu yake ya kwanza inayoitwa Twamaya ambayo ilikuwa na nyimbo 11 ndani yake.

Miongoni mwa ngoma zilizokuwepo kwenye albamu hiyo ni ‘Twamaya’ ambao ni wimbo namba saba kwenye albamu hiyo, ‘Mbuliyo’, ‘Mwandzani’, ‘Truliya’, ‘Swamaha’ ambao amemshirikisha Cheikh MC, ‘Hu Shindiha’ ambao amemshirikisha Chucky Mista Res na nyingine.

KUHUSU KUFUATILIA MUZIKI WA BONGO FLAVA

Dadiposlim ameonekana kuwa mfuatiliaji mkubwa wa muziki wa Bongo Flava hasa ukilinganisha umbali wa Tanzania na nchi ya Comoro siyo mkubwa sana. Lakini pia anaonekana ni mpenzi mkuwa wa WCB kutokana na vile ambavyo amewahi kufanya hapo nyuma.

April 9 ya mwaka huu kwenye shindano hilo la The Voice Afrique linalofanyika nchini Nigeria, msanii huyo aliweza kuimba wimbo wa ‘Show Me’ ambao umeimbwa na Harmonize na Rich Mavoko. Hilo pia limenifanya kuweza kumtaja kama ni mpeniz wa WCB. Hakika sauti yake na uimbaji wake umewavutia watu wengi huku akitolewa macho.

KUHUSU WIMBO WA SIKOMI WA DIAMOND
Hakika ni ukweli usiopingika kuwa baada ya Dadiposlim kuimba wimbo huo ndio amekuwa gumzo kubwa Bongo hasa kutokana na ukubwa wa Diamond na pia ndio aliyeanzisha kwa kuweka vipande vya video ya msanii huyo akiimba wimbo wake huo ambao mwanzoni wakati unatoka haukuonekana kuja kufanya vizuri.

Nilimsikia mtu mmoja aliyekuwa akiangalia video hiyo akisema, msanii huyo ameimba vizuri kuliko Diamond mwenye wimbo wake – Sitaki kujua hilo lakini nachoweza kusema Dadiposlim amejitahidi sana mpaka Diamond aliweza kutumia mtandao wake wa Instagram kwa kumagia sifa.

Kupitia mtandao huo bosi huyo wa WCB aliandika, “Please tag this artist and tell him, am Grateful, and i got too Much Respect for Him!!…🔥🔥🔥 #TheVoiceAfrica #Sikomi.”

“Tell Him Tanzania Loves him and he is Our Winner…..🔥🔥🔥🔥#SIKOMI #TheVoiceAfrica,” Diamond aliandika kwenye video nyingine ambayo aliiweka kwenye mtandao huo.

Hakika Dadiposlim anastahili pongezi kwa kuwa balozi wetu wa muziki wa Bongo Flava japo siyo Mtanzania na sitaweza kushangaa siku moja nikiona msanii huyo akija kufanya kazi na msanii yoyote wa hapa Bongo hakika anaweza kutokana na uwezo wake ambao ameuonyesha kwenye shindano hilo.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents