Mfahamu Sheikah: Mrembo wa Kenya anayefanya muziki uarabuni
Licha ya kuwa na kazi nzuri ambayo Waingereza wanaziita ‘white-color jobs’ yaani kazi za kufanya ukiwa kwenye ofisi nzuri yenye full kiyoyozi, Mercy Wangare aka Sheikah hajakubali kuitupa ndoto yake ya kuwa mwanamuziki mkubwa na wa kimataifa kutoka Kenya.
Akiwa mfanyakazi wa kampuni ya Vodafone jijini Doha, Qatar, Sheikah msichana mrembo, ana miezi minne tu tangu aingie rasmi kwenye muziki na showbiz na kuachia video yake. Licha ya kuwa mpya kwenye midani ya muziki nchini Kenya, video ya wimbo wake wa kwanza, Mali Mbele imeweza kufanya vizuri kwenye vituo vya radio vya Kenya hadi kuingia kwenye Top Ten kwenye baadhi ya vituo hivyo.
Pia video yake hiyo mpaka sasa imeshaangaliwa zaidi ya mara ya 20,000 kwenye mtandao wa Youtube.
Wimbo wake huo umerekodiwa kwenye studio za Calif Records na kwenye video amemtumia mchekeshaji maarufu wa Kenya na muigizaji kwenye tamthilia ya Tahidi High, OJ.
Sheikah ana muonekano wa kuvutia na sio rahisi mwanaume kumwangalia mara moja ukaridhika.
Akiongea na Bongo5 kutoka Doha, Qatar, Sheikah amesema ‘Mali Mbele’ ni kama rasharasha tu kwakuwa mwezi August mwaka huu atarekodi ngoma yake ya pili ambayo anasema itakuwa ni mvua yenyewe.
Ameiambia Bongo5 kuwa licha ya kuwa mfanyakazi, amekuwa akipiga show mbalimbali za waafrika mjini Doha na amejitengenezea jina kubwa huko hivyo mashabiki wa muziki wa Afrika Mashariki wakae mkao wa kula kuona ukali wake live kwenye stage.