Mh. Nassari awasilisha ushahidi mwingine TAKUKURU
Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (CHADEMA) amewasilisha ushahidi mwingine Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuhusu tuhuma za kuhongwa kwa madiwani wa Chama hicho ili kuhamia CCM.
Mhe. Nassari akizungumza na waandishi wa habari leo nje ya ofisi ya Takukuru jijini Dar es salaam amesema kuwa ushahidi alioupeleka leo ni ushahidi wa tatu.
“Tunajiuliza kwa nini Rais hawachukulii hatua DED, DAS au DC wote wa Arumeru kwa kutuhumiwa, watupeleke mahakamani na tungeomba suala hili lichukuliwe kwa uzito wake,” amesema Nassari
Aidha Nassari amesema alitarajia Rais John Magufuli angewachukulia hatua wateule wake wanaohusishwa katika sakata hilo ili kupisha uchunguzi uweze kufanyika kwa uhuru.
Awali Wabunge Lema, Nassari walienda katika Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) kudai kuwa si kweli kwamba madiwani walijiuzulu kwa kile walichoelezwa kumuunga mkono Rais Magufuli, wao walidai wanahongwa waliongozana na Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa ambaye pia alidai jimboni kwake kuna ununuzi wa madiwani.