Miss Tanzania 2009
Mrembo Miriam Gerald kutoka Mwanza kanda ya Ziwa amefanikiwa kutwaa taji la Miss Tanzania kwa mwaka 2009/2010.
Miriam Gerald aliibuka mshindi wa taji hilo usiku wa kuamkia Jumamosi baada ya kuwabwaga warembo wenzake 28 ambao kwa pamoja walikuwa wakigombania taji hilo.
Majaji tisa walimchagua Miriam kuwa Vodacom Miss Tanzania na ataiwakilisha Tanzania katika shindano la urembo la dunia, litakalofanyika baadaye mwaka huu.
Nafasi ya pili ilitwaliwa na Beatrice Lukindo (Vyuo Vikuu) wakati mshindi wa tatu ni Julieth William na Sylvia Shally aliyeshika nafasi ya nne,wote wanaotoka Ilala.
Katika mashindano hayo, shoo nzima ya Miss Tanzania 2009 ilianza saa 4:45 usiku, ilifunguliwa na wasanii wa bongo fleva ambao ni Marlow, Alikiba, Hussein Machozi na Barnabas ambao waliimba wimbo wa pamoja uitwao Umoja Daima.
Ukiacha hayo, Miriam pamoja na kupata tiketi ya urembo ya dunia, pia alizawadiwa Suzuki Grand Vitara lenye thamani ya shilingi milioni 53 na fedha taslimu shilingi milioni tisa pamoja na zawadi ya hereni na kidani cha dhahabu kutoka Tanzanite One na kutwaa taji la mrembo mwenye mvuto kwenye picha na kuzawadiwa Milioni moja.
Saa 7:10 usiku Mwenyekiti wa Miss Tanzania Prashant Patel, alitaja warembo watano ya Miss Tanzania 2009 ambao kati yao walipata mataji mbalimbali ya ubalozi kutoka kwa wadhamini wa shindano hilo.
Katika shindano hilo, Miriam alitangazwa kuwa mrembo mwenye mvuto na Balozi wa Redds pamoja na Sh milioni 1 wakati mrembo mwenye kipaji Tory Oscar ambaye ni Balozi wa Hoteli ya Giraffe anapata sh 500,000 huku Tuzo ya Utalii wa Ndani imekwenda kwa Sia anayepa Sh2.1mil na kompyuta ya sh1.2mil.
Mbali na mataji hayo, mshindi wa pili ameondoka na sh6.2milioni, wakati mshindi wa tatu sh4mil huku mshindi wa nne akipata sh3mil. Mshindi wa tano Sh2.4 mil wakati wa sita hadi wa 10 kila mmoja anapata sh1.4mil. Walioshika nafasi ya 11 hadi 29 kila mmoja ameondoka na sh700,000.
Timu nzima ya Bongo5 inamtakia mafanikio mema mrembo Miriam katika kuliwakilisha taifa.