Miss Tanzania na bosi wa zamani wa TRA wachekelea uamuzi wa Mahakama Kuu
Mahakama Kuu jijini Dar es Salaam, Ijumaa hii imetupilia mbali rufaa ya Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka(DPP) dhidi ya aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya na wenzake wawili.
Mahakama hiyo imeitaka Jamhuri inayowashtaki watatu hao kurudi mahakama ya hakimu mkazi Kisutu kufanya marekebisho ya shtaka hilo.
Wengine waliopo kwenye kesi hiyo ni waliokuwa wafanyakazi wa benki ya StanBic Tanzania, Sioi Sumari na Miss Tanzania wa zamani, Shose Sinare.
Jumanne hii Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilisema jalada la kesi inayowakabili watatu hao bado lipo Mahakama Kuu na kwamba washtakiwa hao walitakiwa kwenda mbele ya Jaji Mfawidhi kwa maelekezo mengine.
Hayo yalisemwa na Hakimu Mkazi, Emilius Mchauru pale kesi ya washtakiwa hao ilipokuja kwa ajili ya kutajwa baada ya mawakili wa pande zote mbili kusema kuwa kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kupata maelekezo kutoka Mahakama Kuu kama ilivyoamuliwa mara ya mwisho.
Siku chache zilizopita washtakiwa hao walifutiwa shtaka la utakatishaji fedha.
Bado wanakabiliwa na mashtaka mengine saba.
Baada ya kufutiwa shtaka hilo, DPP aliwasilisha hati ya mapendekezo ya kukata rufaa ya kupinga uamuzi wa kufuta shtaka namba nane la utakatishaji fedha linalowakabili watuhumiwa hao.
Hiyo ilipelekea pia zoezi la dhamana kugonga mwamba.
Hatua hiyo imewapa mashaka wananchi wengi kuhusu kama Jamhuri inaweza kushinda kesi hiyo dhidi ya washtakiwa hao.
“Hawa wanasheria wa serikali wanashindwa kusimamia kesi coz wanajua hata serikali isiposhinda kesi wao hawana hasara hasara ni kwa serikali kodi zetu zinakosa kufanya maendeleo ya taifa ni kulipa madeni tu,” ameandika mwananchi mmoja kwenye Facebook.
“Haya kikwete alilalamika sana kwa nn serikali anashindwa kesi nyingi magufuli naye the same.usione MTU jaji au wakili Wa serikali ukadhani ni professional ktk eneo hilo wala kumbe alitakiwa kufanya kazi nyingi ila ndo hivo kujuana rushwa ikasababisha ili mradi Siku zinaenda,” ameandika mwingine.