Miss World kufanyika Tanzania?
Kampuni ya Lino International Agency,
inayoandaa shindano la kumsaka Miss Tanzania, imesema inakusudua kutuma
maombi ya kuandaa mashindano ya urembo ya dunia
Akizungumza
jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hashim Lundenga,
alisema hivi karibuni kuwa, wamepanga kutuma ujumbe maalumu jijini
Laondon, Uingereza yalipo makao makuu ya waandaaji wa shindano hilo.
Lundenga alisema kuwa wamefikia hatua hiyo baada ya kujiridhisha kuwa
wanaweza kufanya hivyo, hatua ambayo pia iliungwa mkono na wadhamini
wakuu wa Miss Tanzania, Kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom.
“Tumekuwa na wazo hilo la kuandaa mashindano kwa muda mrefu baada ya
kuona tuna uwezo huo, lakini tumepata nguvu zaidi baada ya wadhamini
wetu (vodacom) kukubaliana na wazo letu hilo”, alisema Lundenga.
Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa wanajua itachukua muda mrefu mpaka
maombi yao kukubaliwa kutokana na sera za waandaaji wa Miss World
kutotabirika imebidi watume ujumbe hilo kisha kusubiri hatima yao.
Aliongeza kuwa mchakato wa Tanzania kuwa wenyeji wa mashindano ya dunia
unaonyesha utakuwa mrefu kutokana na shindano hilo kufanyika mara
nyingi zaidi katika nchi za Bara la Afrika, tofauti na mabara mengine.
Baadhi ya nchi hizo ni pamoja na Afrika Kusini ambayo imeandaa shindano
hilo zaidi ya mara tano tangu kuanza kwa mashindano hayo mwaka 1954.