Habari

Mjamzito afanyiwa ukatili na mumewe

MWANAMKE mwenye ujauzito wa miezi minane, mkazi wa Kijiji cha Mseki, wilayani hapa, Victoria Simon (27), amechomwa visu na mumewe na kusababisha kichanga kilichokuwa tumboni kufariki dunia.

na Patrick Mabula

 

MWANAMKE mwenye ujauzito wa miezi minane, mkazi wa Kijiji cha Mseki, wilayani hapa, Victoria Simon (27), amechomwa visu na mumewe na kusababisha kichanga kilichokuwa tumboni kufariki dunia.

 
Victoria alishambuliwa kwa kuchomwa visu sehemu mbalimbali mwilini na mumewe aliyefahamika kwa jina la Mahano Rwambo. Tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki iliyopita kijijini hapo na kwamba chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa kimapenzi.

 
Akisimulia tukio hilo katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama alikolazwa mwanamke huyo, dada yake, Felister Kazige alisema mdogo wake alikuwa ameolewa na Rwambo na tayari walikuwa na watoto wawili na walikuwa wakiishi Ushirombo, wilayani Bukombe.

 
Alisema kutokana na kukorofishana na mumewe, mdogo wake huyo alirudi kwao Mseki na kwamba siku ya tukio Rwambo alikuwa amemfuata.

 
“Ilipofika saa mbili usiku, alimwambia mkewe amsindikize kwa Mwenyekiti wa Kitongoji akajitambulishe, lakini walipokuwa njiani, ghafla alianza kumshambulia kwa kisu,” alisema dada huyo.

 
Akizungumza kwa tabu katika wodi ya wazazi alipolazwa, Victoria alisema wakati wakielekea kwa Mwenyekiti wa Kitongoji mumewe alikuwa kimya na ghafla alimrukia na kuanza kumkata kisu tumboni hadi utumbo ukatoka.

 
Alisema kuwa mwanamume huyo pia alimkata shingoni, mikononi, shavuni na puani na kwamba alipopiga mayowe alikimbia.

 
Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya, Dk. Yesaya Membe, alisema mwanamke huyo aliokolewa na gari la Mbunge wa Kahama, aliyekuwa katika ziara sehemu hiyo kutoka Kituo cha Afya cha Kata ya Burungwa alipokuwa amepelekwa baada ya kumchukua na kumkimbiza hadi wilayani.

 
Dk. Membe alisema alipofikishwa hospitaini hapo, walimshona majeraha yake na baadaye waliendelea kumfanyia uchunguzi na ndipo walipogundua mtoto aliyekuwa tumboni alikuwa amefariki. Afya ya mwanamke huyo inaendelea vizuri.

 
Polisi wilayani hapa wamethibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kwamba wanaendelea kumsaka mwanamume huyo.

 
Source: Tanzania Daima

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents