Michezo

Mourinho amuita Pogba ‘kirusi’ wa Manchester United mbele ya wachezaji wenzake

Jose Mourinho amemshutumu Paul Pogba na kusema ni kirusi kinachochafua hali ya hewa kwenye kikosi chake cha Manchester United, baada ya sare ya 2-2 dhidi ya Southampton kwenye Ligi Kuu England juzi Jumamosi.

Mourinho amemshambulia Pogba kwa maneno makali mbele ya wachezaji wenzake kwenye vyumba vya kubadilishia huko uwanjani St Mary’s.

Chanzo cha habari hiyo kilifichua kikisema: “Jose alimwita Pogba kuwa ni kirusi mbele ya wachezaji wote. Alimwambia Pogba ni kama mtu mwenye virusi vya mafua kwenye chumba kilichofungwa milango, ukipita tu unaambukizwa.’

“Amemwambia hachezi, haheshimu wachezaji wenzake na mashabiki na amekuwa na mtazamo hasi kwa watu wanaomzunguka klabuni hapo.”

Kauli hizo zinadaiwa kuamsha hisia za kwamba, huenda kiungo huyo aliyenaswa kwa Pauni 89 milioni asiendelee kuwapo kwenye kikosi hicho cha Old Trafford, baada ya msimu huu kumalizika ama kuomba kuondoka.

Kwenye hatua nyingine, Kocha Mourinho amevichenjia vyombo vya habari kwamba, vimekuwa vikimfuatilia sana na kumtengenezea ugomvi na wachezaji wake hata kama jambo kama hilo halipo. Kocha huyo Mreno alisema wapinzani wake Pep Guardiola, Jurgen Klopp na Maurizio Sarri wamekuwa hawana presha kabisa na wanaishi maisha ya raha tofauti na yeye.

“Mmekuwa mkiuliza kila wakati mchezaji wa Man United asipocheza, lakini mtavumisha kitu tu. Siku zote mtakuja kusema kuna tatizo la kinidhamu, kuna tatizo na kocha. Mtasema mara oooh mchezaji kagombana na kocha, hayo yote yapo hapa Man United,” alisema Mourinho.

“Huko Chelsea, Willian asipocheza hakuna tatizo Willian na Kocha Sarri. . Inaonekana kuwa ni kawaida tu. Huko Liverpool, Fabinho na Keita wasipocheza, wanampenda Jurgen Klopp na Jurgen anawapenda? Acheni hizo,” aliwaka.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents